KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimesema kinaunga mkono mapendekezo ya Kikosi Kazi cha Kuratibu Maoni ya Wadau wa Demokrasia ya Vyama vya Siasa, ya mchakato wa ulatikanaji katiba mpya kuanza baada ya 2025. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumanne, tarehe 22 Machi 2022, jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga.
Henga amesema, 2025 sio mbali kwa kuanza mchakato huo, huku akipongeza hatua ya Rais Samia kuruhusu marekebisho hayo kufanyika kitendo ambacho kilipingwa na mtangulizi wake, Hayati John Magufuli.
“Lengo ni mchakato wa katiba ufufuliwe bila kujali muda, hapo nyuma hatukujua unaanza lini lakini sasa hivi umefufuliwa. 2025 sio mbali unaweza kuwa muda mzuri,” amesema Henga.
Alipoulizwa kama LHRC ina imani na kikosi kazi hicho, Henga amesema “Tunaimani nacho sababu kilipoteuliwa kimeteuliwa kwa kuchukua wajumbe kutoka kada tofauti. Hatujaona mrengo wa wanasiasa, hakijaegemea mrengo fulani. Mwenyekiti wake ni mwanataaluma.”
Kikosi kazi hicho kiliundwa mwishoni mwa 2021, kwa ajili ya kufanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na washiriki wa mkutano wa wadau wa vyama vya siasa, uliofanyika jijini Dodoma Desemba mwaka jana, kwa ajili uboreshaji sheria na katiba.
Leave a comment