KESI ya kimkataba kati ya Feisal Salum (Fei Toto) dhidi ya klabu ya Yanga itasikilizwa kwa saa 3 na kamati ya Sheria na Hadhi za wachezaji kwenye makao makuu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania TFF. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Pande zote mbili zilifika leo mapema katika ofisi za makao makuu ya shirikisho hilo, zilizopo Karume, Ilala jijini Dar es Salaam, mara baada ya kupokea wito.
Licha ya kufika mapema lakini shauri hilo lilipangwa kuanzia kusikilizwa majira ya saa 9 kamili jioni ambapo Feisal anawakilishwa na mawakili wake wawili Makubi Kunju na Ndurumah Majembe kutoka Fortis Attorneys.
Kwa upande wa Yanga wao kwenye kesi hiyo wanaongozwa na mtendaji Mkuu wa klabu hiyo Adrew Mtine sambamba na Wakili Simoni Patrick.
Katika kesi hiyo upande wa Yanga utatumia Saa 1 kuwasilisha nyaraka zao mbele ya kamati hiyo, ambapo upande wa Fei Toto ukiongozwa na mawakili wake nao utatumia Saa moja kujibu hoja hizo.
Mara baada ya ungwe hiyo ya kwanza, upande wa Yanga utatumia tena nusu saa kufanya majumuisho, na dakika 30 zilizosalia zitatumika kwa maswali.
Leave a comment