MARA baada ya kuingia mkataba hivi karibuni wa kuwa mdhamini mwenza wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kampuni ya Gsm Group imeonesha nia tena ya kudhamini Ligi daraja la kwanza (Championship) mara baada ya kukosa udhamini kwa muda mrefu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Akithibitisha hayo, mkurugenzi wa uwekezaji wa kampuni ya hiyo Mhandisi Hersi Said amesema kuwa kampuni hiyo ipo katika hatua ya mwisho ya kuona namna gani watakavyoweza kudhamini Ligi hiyo.
“Tumekuwa tukipata maombi mengi kama Gsm kudhamini Ligi daraja la kwanza, tupo hatua za mwisho kama Gsm kuona jinsi tutakavyosapoti Ligi daraja la kwanza na la Pili.” Alisema Hersi
Hersi ameyasema hayo kwenye mkutano wa Baraza kuu la bodi ya Ligi, uliofanyika mkoani Morogoro, huku kukiwa na ajenda kuu moja ya uchaguzi wa bodi hiyo kwa nafasi ya mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wa bodi.
Aidha Hersi aliendelea kusema kuwa wataangalia udhamini huo katika jicho la uweledi bila kutikiswa na maneno ya watu na muda sio mrefu watakamilisha suala hili.
“Sisi ni watu imara, hatuwezi kutikiswa kwa maneno, tutaliangalia hili jambo kwa uweledi na muda sio mrefu tutarudi mezani kumaliza hili la Ligi daraja la kwanza.” Aliongezea kiongozi huyo
Kwenye udhamini wa Ligi Kuu kampuni hiyo ilitoa kiasi cha shilingi bilioni 2 kwa mkataba wa miaka miwili, na kutimiza idadi ya wadhamini wanne kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu huu.
Leave a comment