MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Dk. Philip Mpango amewaasa wazazi na walezi kulea watoto wao kwa kuzingatia maadili mema ya kitanzania pamoja na kuwa makini na maudhui ya watoto (katuni) katika televisheni ili kuwaepusha na kujifunza mambo yasiofaa. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea)
Pia amewataka walimu wa shule za msingi, sekondari na hata vyuoni kukemea kwa nguvu uharibifu wa maadili ya kitanzania katika maeneo ya kutolea elimu.
Dk. Mpango ametoa kauli hiyo leo tarehe 09 Aprili 2023 alipoungana na waumini wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Mwenyeheri Maria Theresa Ledochowska Kiwanja cha Ndege Dodoma katika Ibada ya Jumapili ya Sikukuu ya Pasaka.
Akizungumza na waumini wa Kanisa hilo mara baada ya kumalizika kwa Ibada, Dk. Mpango ambaye pia alikuwa ameambatana na mkewe Mama Mbonimpaye Mpango, amewasihi wazazi na walezi kuwalinda watoto pamoja na vijana wao dhidi ya matumizi mabaya ya simu pamoja na kufuatilia mienendo yao wakati wote.
Makamu wa Rais amesema ni vema kwa wazazi kutambua marafiki wa watoto wao na kuwapa miongozo sahihi wakati wote na kutowaacha kujiongoza wenyewe.
Aidha, Makamu wa Rais amewaasa waumini na watanzania kwa ujumla kuongeza jitihada katika ulinzi na uhifadhi wa mazingira kwa kupanda miti katika kila kaya pamoja na usafi katika maeneo yao. Amesema ni vema wazazi kutoa mafunzo kwa watoto wao namna ya kupanda miti na kuisimamia.
Leave a comment