MBUNGE wa kuteuliwa na Rais, Dk. Bashiru Ally, ameitaka Serikali kuja na mikakati ya kutatua changamoto ya mfumuko wa bei za vyakula huku akisema kwamba njaa inadhalilisha heshima ya uhuru wa nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Dk. Bashiru ameyahoji hayo leo tarehe 31 Januari 2023, bungeni jijini Dodoma.
“Njaa inadhalilisha heshima ya uhuru wa nchi, njaa inatweza utu wa binadamu. Kwa hiyo tatizo la mfumuko wa bei za vyakula ni tatizo ambalo tutake tusitake lazima tuongeze kiwango cha ubunifu kukabiliana nalo,” amesema Dk. Bashiru.
Mbunge huyo amedai kuwa, kuna baadhi ya wananchi wameanzisha utaratibu wa kupata milo miwili kwa siku badala ya mitatu kama ilivyozoeleka ili kumudu gharama za vyakula.
“Nilikuwa nazungumza na baadhi yao mmoja anasema wamepanga milo kwa kupiga pasi kwa maana kwamba asubuhi na chakula cha mchana vinaunganishwa kwenye majira ya saa 5 na 6 asubuhi, halafu mlo wa usiku unaunganishwa kati ya saa 11 na 12 jioni, hawasubiri kujadili mambo ya Ukraine na tabia ya nchi,” amesema Dk. Bashiru.
Dk. Bashiru amesema “kama wameanza kuchukua hatua wananchi wanakabiliana na hali hiyo nchi ianenda maendeleo yanaendelea hatujasimama, kwa nini Serikali isipanue wigo wa kufikiri na ubunifu kukabiliana na njaa?”
Katika hatua nyingine, Dk. Bashiru amehoji jitihada za Serikali katika kupunguza mfumuko wa bei za bidhaa hususan vyakula, zimezaa matunda gani, huku akihoji kwa nini haidhibiti uuzaji holela wa mazao ya vyakula nje ya nchi.
“Nimalize kwa kuacha maswali machache, je ruzuku ya mbolea , mafuta na mbegu umepunguza ukali kiasi gani ya mfumuko wa bei ya vyakula. Je, kutokuwa na karantini kumepunguza kiasi gani makali ya mfumuko wa bei za vyakula. Je, udhibiti wa kuuza vyakula nje ukiwepo unamnufaisha nani na pia vyakula vikiuzwa nje kwa uwazi hiyo ruksa inamnufaisha nani?” amehoji Dk. Bashiru.
Aidha, Dk. Bashiru ameishauri Serikali kuwatengezea mazingira bora ya uzalishaji wakulima, wavuvi na wafugaji ili wazalishe chakula kwa wingi kwa ajili ya kudhibiti mfumuko huo.
Akielezea athari zinazowakabili wananchi kutokana na mfumuko huo, Dk. Bashiru amedai baadhi yao wanapata mlo mara mbili kwa siku kutokana na kushindwa kumudu gharama za vyakula kutokana na kipato chao kuwa kidogo.
Serikali inatoa ruzuku katika mbolea, mbegu na mafuta izi kupunguza gharama kwa wakulima. Halafu mazo yao wanayauza nje ya nchi
Fedha zetu za tozo na kodi zinasaidia nchi za jirani wakati wananchi wetu wanaishi na njaa. HUU NI WIZI