JESHI la Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limeanza uchunguzi wa video ya ngono, inayosambazwa kwenye mitandao ya kijamii inayodaiwa kuwa ni ya Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Kamanda wa Jeshi la Polisi, Kanda ya Dar es Salaam, Kamanda Lazaro Mambosasa wakati akizungumza na wanahabari leo tarehe 8 Mei 2019 jijini humo.
Kamanda Mambosasa amesema, Jeshi la Polisi la kanda hiyo kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), limeanza uchunguzi wa video hiyo.
Kamanda Mambosasa amesema, Askofu Gwajima sio mtuhumiwa wa usambazaji huo kama baadhi ya watu wanavyodhani na kwamba, ni muathirika wa tukio hilo, hivyo amewataka wananchi kuacha kusambaza video hiyo kwa kuwa ni kosa la jinai.
“Jeshi la Polisi limeanza uchunguzi wa video hiyo ya ngono mara moja na linapenda kuwataarifu wananchi kwamba Askofu Gwajima sio mtuhumiwa bali ni muathirika wa tukio hilo kwani jambo hili linaweza kufanywa na mtu yeyote kwa nia ya kumharibia heshima yake kwa jamii na waumini wake,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda Mambosasa amewataka waumini wa Askofu Gwajima kuwa watulivu wakati uchunguzi wa tukio hilo ukiendelea kufanywa na Jeshi la Polisi, ili kubaini aliyesambaza video hiyo na lengo la kufanya hivyo.
Leave a comment