Mkuu wa Wilaya ya Ileje mkoani Songwe, Farida Mgomi amemuagiza Afisa Uchaguzi wilayani hapa, Veronica Michael kuwapa mwongozo wananchi wa Kijiji cha Luswisi Kata ya Luswisi namna ya kupata viongozi wa Halmashauri ya Kijiji hicho baada ya viongozi wa awali kufukuzwa na wananchi waliowatuhumu kwa matumizi mabaya ya madaraka. Anaripoti Ibrahim Yassin. Songwe…(endelea)
Mgomi ametoa agizo hilo mwishoni mwa wiki katika mkutano wa hadhara wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi kijijini hapo baada ya kupokea taarifa ya kijiji ya kutokuwepo kwa Mwenyekiti wa Kijiji na halmashauri ya Kijiji tangu Machi mwaka huu.
Aidha, Mgomi amesema kutokuwepo kwa wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji kumesababisha kijiji kukosa maendeleo kwani viongozi muhimu wa kuibua vipaumbele hawapo hali ambayo imedumaza maendeleo ya kijiji.
Mgomi amesema ili kuhakikisha shughuli za maendeleo zinatekelezeka amemuagiza afisa uchaguzi kuhakikisha anatoa mwongozo mapema ili wananchi wapate viongozi wa mpito ambao wataongoza mpaka 2024 ambao ni mwaka wa uchaguzi.
“Nishauri wananchi hakikisheni mnafanya maamuzi ambayo hayatakigharimu kijiji chenu kimaendeleo, kwani mpaka sasa maendeleo yamesimama onesheni ushirikiano na viongozi wa mpito mtakaowachagua kwa mwongozo mtakaopewa na Afisa Uchaguzi ili mwaka 2024 mkachague viongozi sahihi kwa mustakabali wa kijiji,” amesema Mgomi.
Kwa upande wake Afisa Uchaguzi wilayani hapa Veronica Michael amesema atayafanyia kazi maagizo ya mkuun huyo wa wilaya ili wananchi hao wapate viongozi ambao wataongoza kwa masilahi ya Kijiji hicho.
Leave a comment