MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (Dawasa), imewataka wakazi wa maeneo ya Goba, Tegeta, Madale, Mivumoni na Salasala kutosikiliza maneno ya wanasiasa wanaopotosha juu ya upatikanaji wa huduma ya maji ili kujipatia kura. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Dawasa imesema, baadhi ya wanasiasa wanataka kutumika suala hilo kama mtaji wa kujipatia kura katika kipindi hiki cha kampeni za Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
Kampeni za uchaguzi huo zimekwisha kuanza tangu tarehe 26 Agosti na zitahitimishwa 27 Oktoba 2020.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa, Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema, wanaendelea na usogezaji wa huduma za maji kwa wananchi “lengo la Dawasa ni kuhakikisha Jiji la Dar es Salaam na Pwani wanapata maji kwa asilimia 100.”
Mhandisi Luhemeja amesema, Dar es Salaam kwa sasa inapata maji kwa asilimia 88 na “ndani ya miaka miwili ijayo, kila wilaya tutakuwa na upatikanaji ya kutosha.”
Mhandisi Luhemeja ameongeza kuwa, wananchi wanavyozidi kulipa fedha ndivyo inawasaidia Mamlaka kupata fedha za kutekeleza miradi mbalimbali ya majisafi na majitaka
“Wanavyozidi kulipa, inatusaidia sisi kufikisha huduma za maji kwenye maeneo yenye changamoto za maji kupitia fedha za ndani” alisema Luhemeja.
Kuhusu wanasiasa, Mhandisi Luhemeja amesema “kumekuwapo na upotoshaji mwingi hasa kipindi hiki cha kampeni, tuwatoe wasiwasi wananchi na tuwahakikishie maji yanakuja.”
“kupitia mradi wa uboreshaji maji kuanzia Chuo kikuu hadi Bagamoyo unaofadhiliwa na banki ya dunia , tayari tumeshaanza utekelezaji kwa kulaza mabomba eneo la Mabwepande na tunaelekea maeneo ya salasala , wazo na maeneo mengine. watu wasiwapotoshe, Serikali ipo na Dawasa ipo maji watapata,” amesema Mhandisi Luhemeja
Ofisa mtendaji mkuu ameongezea kuwa, kwa miaka mitano ya Serikali inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli wamekuwa wakipambana kuboresha mtandao wa maji, kuongeza mapato na imesaidia sana kuongeza mtandao wa maji.”
Mhandisi Luhemeja ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wananchi wanaohudumiwa na Dawasa ambao ni mikoa ya Dar es Salaam na Pwani kwani wamekuwa msaada mkubwa kwa uendeshaji wa Mamlaka
“Kipindi cha nyuma, watumiaji walikuwa hawalipi sana huduma ya maji, tulikuwa hadi tuwasitishie huduma na mara nyingine kutumia ubabe lakini kuanzia mwaka 2015 wakati nakabidhiwa shirika hadi sasa hali imebadilika sana.”
“Mwitikio umekuwa mkubwa na namna tunavyokusanya madeni, hawasumbuwi kama zamani na zaidi niwaombe wasituache. Tunavyokusanya ndivyo tunapata fedha za kuongeza ufanisi wa kusogeza huduma sehemu nyingine,” alimaliza Mhandisi Luhemeja
Leave a comment