CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimemtaka Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kutekeleza ahadi yake ya kuunda baraza la vijana la taifa, ili kundi hilo lipate jukwaa la kusemea matatizo yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Ijumaa na Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, kupitia ukurasa wake wa Twitter, akizungumzia kilele cha wiki ya vijana taifa, kinachotarajiwa kufanyika kesho tarehe 14 Oktoba 2023.
“Nikukumbushe pia Rais @SuluhuSamia ahadi yako Mwanza ya tarehe 15 Juni 2021 ya kuhakikisha na kuharakisha #BarazaLaVijana kuundwa ambalo ulilitaja kuwa ni hitaji la muda mrefu la vijana,” ameandika Mnyika.
Mbali na uundwaji wa baraza hilo, Mnyika amewataka vijana kupaza sauti zao kudai mazinira mazuri na mifumo yenye kuongeza ajira.
“Lakini zaidi muungane na makundi rika mengine kudai katiba mpya na uchaguzi wa haki. Utajiri wa taifa letu ni pamoja na uwingi, nguvu na ubunifu wa vijana ambao ni kati ya rasilimali watu kuu. nawahimiza mjitambue na muwe tayari na uthubutu wa kufanya ambayo yataacha alama ya ujana wenu,” ameandika Mnyika.
Leave a comment