CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema hakitasita kuanzisha hoja au ajenda ya kuhakikisha wote (wakuu wa mikoa, wilaya) wanaokiuka maelekezo ya namna ya kuwapanga wamachinga, wanaondolewa katika nafasi zao kuliko kuwaacha wakizalisha athari hasi katika jamii. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Pia kimetangaza kuanza kuziwajibisha kamati za siasa za mikoa na wilaya ambazo zitazembea au kulegalega kuhusu operesheni hiyo na kusababisha isiende kwa mafanikio kama ambavyo Mwenyekiti wa CCM na Rais Samia Suluhu Hassan ameagiza.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2021, Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Shaka Hamidu Shaka wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Shaka amezungumzia kuhusu mwenendo wa operesheni inayoendeshwa na wakuu wa mikoa ya kuwapanga ma kuwahasha wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama ‘wamachinga’ katika mikoa yote nchini.
Amesema CCM inafuatilia kwa ukaribu zoezi hilo katika maeneo mbalimbali nchi nzima na katu haitakubali wala kuachia liendeshwe kinyume na maamuzi na maagizo ya Rais Samia.
Aidha, amesema Chama kinawakumbusha viongozi na watendaji wa serikali kuwa uamuzi wa serikali uliotangazwa na Rais Samia wa kuwapanga na kuwahamisha wamachinga uliwekewa msisitizo na kuhakikisha maeneo wanayopangiwa au kuhamishiwa yanakuwa yameandaliwa kuwekewa miundombinu rafiki kutekeleza shughuli za machinga na wateja wao bila kukwamisha fursa za kujitafutia kipato.
“Mfano jana pale mbezi – kimara maeneo ya jioni kuna watu walikuwa wanapita na vipaza sauti vyao vya kuwataka machinga wahame, tunajiuliza saa 12 jion unamwambia mmachinga ahame, anakwenda wapi?
“Tulifuatilia kwa kina na kujua wengi wao wamechukua mitaji yao na kwenda majumbani mwao kutafakari jambo hili ambalo kiubinadamu halikuwa jambo zuri. Hata stendi ya Maguful imejaa.
“CCM inawaelekeza wakuu wa mikoa, wilaya na wote wenye mamlaka katika kusimamia maelekezo ya Rais, wanachukulia suala hili kwa ufanisi na mafanikio makubwa,” amesema.
Aidha, amempongeza Mkuu wa mkoa wa Arusha, John Mongela amefanya vizuri hivyo kuna haja ya maeneo mengine kujifunza kutoka kwake.
“Baada ya kufuatilia kwa karibu utekelezaji na uamuzi huo wa kisera, Chama kinaelekeza kuwa kitendo cha kuwahamisha machinga bila ya kuwaandalia maeneo mbadala ambayo yameboreshwa kwa kuwekewa miundombinu kwa ajili ya shughuli zao, ni marufuku na hakikubaliki.
“Kwenye hili chama kitasimamia ipasavyo, kinazikumbusha kamati za siasa za mikoa, na wilaya kwamba kwenye jambo hili kama tulivyozungumza kwenye ilani chama kina masilahi mapana,” amesema.
Amesema kwa mujibu wa katiba ya CCM, Mkuu wa mkoa, wilaya ni wajumbe halali wa kamati za siasa za mkoa na wilaya, hivyo mamuzi na maelekezo hayo ni vema mashauriano yakafanyika baina ya chama na serikali za mikoa ili wote kwa pamoja kufanikisha jambo hili kwa mafanikio.
Leave a comment