WAKATI waumini wa dini ya Kiislamu wakiendelea na mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani, Benki ya NMB imejumuika na wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na watoto wenye mahitaji maalum Dodoma kupata futari ya pamoja. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma… (endelea).
Hafla hiyo iliongozwa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Tulia Ackson na ujumbe wa Benki ya NMB ulioongozwa na Mwenyekiti wa Bodi – Dk. Edwin Mhede pamoja na Afisa Mkuu wa Fedha, Juma Kimori aliyemuwakilisha Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki.
Katika hafla hiyo, Benki ya NMB ilitoa msaada wa vyakula kwa vituo viwili vya watoto yatima Dodoma, vilivyokabidhiwa na Spika Tulia.
Akizungumza katika hafla hiyo, Spika Tulia amesema: “Tunaithamini sadaka hii, tunawapongeza NMB kwa kazi nzuri, na hii ni kwa niaba ya wote waliofuturu hapa na ambao hawawezi kupata fursa ya kuongea, naomba mfahamu tu kuwa tunaheshimu sana sadaka hii mliyoitoa leo hapa na kule kote mlikofuturisha.
“Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu ameeleza hapa maeneo mbalimbali mlikopita kufuturisha jamii ya wenye uhitaji wakiwemo watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu, viongozi wa serikali na wateja wenu, tunawapongeza na kuwashukuru sana kwa hili,” amesema Dk. Tulia.
Leave a comment