SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kutoa mafunzo ya udhibiti wa sumukuvu kwenye mahindi, karanga na bidhaa zake katika wilaya za Kiteto, Kongwa, Gairo na Kilosa kwa wasafirishaji, wafanyabiashara na wasindikaji wa mazao hayo zaidi ya 600. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Mafunzo hayo ambayo yaliyoanza kutolewa na TBS kwenye wilaya hizo kuanzia tarehe 31 Mei mwaka huu na yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 14 Juni mwaka huu.
Mafunzo hayo yanatolewa na shirika hilo kupitia Mradi wa Kitaifa wa Kudhibiti Sumukuvu ujulikanao kama Tanzania Initiative for Preventing Aflatoxin Contamination (TANIPAC).
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa mafunzo hayo, Jabir Abdi, ambaye ni Mwenyekiti wa mradi huo TBS, alisema mafunzo hayo yatawasadia wafanyabiashara na wasindikaji wa mahindi na karanga kupata masoko ya uhakika na kuwezesha wananchi kuepukana na madhara ya kiafya yatokanayo na sumukuvu.
Alisema mafunzo hayo yametolewa kwenye wilaya hiyo kutokana na tafiti za awali za mradi huu kubaini wilaya hizo kuwa miongoni mwa maeneo yenye changamoto ya uwepo wa sumukuvu katika mnyororo wa thamani wa mazao ya mahindi, karanga na bidhaa zake.
Abdi alitaja faida za mafunzo kuwa yalenga kulinda afya za binadamu, kuwezesha biashara ya mazao ya mahindi na karanga, kulinda afya za mifugo na kuwezesha utoshelevu wa chakula salama.
Kwa mujibu wa Abdi faida nyingine za mafunzo hiyo ni kuwawezesha wadau katika mnyororo wa karanga, mahindi na bidhaa zake kuhimili ushindani katika masoko ya ndani, kikanda na nje ya nchi.
Alifafanua kwamba mafunzo hayo ni muhimu kwa sababu usalama wa chakula unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na uchafuzi wa sumukuvu ambao husababisha madhara ya kiafya na hata kiuchumi.
Alisema sumukuvu huathiri zaidi mazao ya mahindi na karanga ambayo ni sehemu muhimu ya chakula cha Watanzania hapa nchini.
“Kwa sababu hiyo sisi sote tunatakiwa kuzingatia mikakati ya kukabiliana na sumukuvu ili vyakula vyetu viendelee kuwa salama kwa muda wote,” alisisitiza Abdi.
Alifafanua kwamba TBS inatambua nafasi ya wafanyabiashara, wasindikaji na wasafirishaji kwa ujumla na mchango walionao, hivyo TANIPAC imeandaa mafunzo hayo mahususi kupitia TBS ili kuwajengea uwezo kwa ajili ya udhibiti sumukuvu.
Alisema umuhimu huu unasabishia suala la usalama wa chakula kupewa kipaumbele katika kulinda afya, jamii na uchumi wa nchi, kwa kuwa ndiyo kigezo muhimu cha biashara kitaifa na kimataifa.
Alihimiza wadau hao kuzingatia mambo muhimu yanayoshauriwa na wataalam ili kudhibiti sumukuvu katika chakula, ikiwa ni pamoja na kuzingatia kanuni bora za kilimo kama inavyoshauriwa na wataalam, kuvuna na kuondoa shambani mahindi na karanga mara baada ya kukomaa vizuri na kukaushia vizuri mazao yaliyovunwa kabla kuhifadhi.
Nyingine ni kuepuka kurundika mazao moja kwa moja kwenye sakafu, kuhakikisha wanahifadhi vizuri mazao kwa lengo la kuepuka wadudu waharibifu, wanyama, joto kali na unyevunyevu.
Leave a comment