JOB Ndugai, aliyekuwa Spika wa Bunge la Jamhuri, amewataka watu wenye ulemavu kufika katika halmashauri ili wapewe asilimia mbili za mapato kwa mujibu wa sheria. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Wito huo umetolewa tarehe 17 Agosti 2020 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Kimataifa wa Viongozi, Demokrasia na Uchumi dhidi ya watu wenye ulemavu uliofanyika kitaifa jijini Dodoma.
Ndugai, mbunge wa Kongwa ambaye anamaliza muda wake amesema, watu wenye ulemavu wanatakiwa kujitokeza kushiriki katika fursa mbalimbali za maendeleo, badala ya kukaa majumbani au kuishi maisha ya hofu.
Akizungumza na viongozi wa vyama vya watu wenye ulemavu kutoka Tanzania Bara pamoja na Visiwani, pia wadau mbalimbali amesema, watu wenye ulemavu wana haki sawa na watu wengine.
Amesema, mila na desturi za kitanzania bado zinawakandamiza watu wenye ulemavu kwa kuwaona kama vile hawafai kupata haki zao.
“Wote mnajua, bado mila na desturi za baadhi yetu zinaendelea kuwakandamiza watu wenye ulemavu, kwa kuwaona hawana haki ya kupata elimu au kujitegemea katika kufanya kazi zao.
“Kutokana na hali hiyo, naomba niwaambie nyie viongozi mliofika katika mkutano huu, ni lazima kuhakikisha mnatoa elimu kwa jamii kuwa kitendo cha mtu kuwa mlemavu, hakimuondolei haki yake ya elimu, uchumi au uongozi,” amesema Ndugai.
Peter Charles, Mshauri wa Masuala ya Watu Wenye Ulemavu Tanzania amesema, mkutano huu unalenga kuwajengea uwezo watu wenye ulemavu ili waweze kujua haki zao.
Na kwamba, mkutano huo unawashirikisha viongozi wote kutoka kwenye vyama vya watu wenye ulemavu ili kuwajengea uwezo juu kutambua, uongozi, demokrasia na uchumi kwa watu wenye ulemavu.
“Kutokana na hali hiyo, katika mkutano huu watakaotoa mada mbalimbali ni watu wenye ulemavu ambao wamekuwa wakifanya kazi za moja kwa moja serikalini, huku wakifanya kazi vizuri na za kuvutia na kuonesha jamii kuwa watu wenye ulemavu ni watu ambao wapo makini na sahihi,” amesema Charles.
Leave a comment