CONSTATINE Kanyasu, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii ameitaka Bodi mpya ya magavana wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori (Mweka), kuhakikisha wanatoa mafunzo yenye ubora na kukidhi mahitaji kulingana na vipaumbele vya Taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Moshi … (endelea).
Kauli hiyo imetelewa wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Magavana iliyofanyika katika chuo hicho, mkoani Kilimanjaro. Waziri Maliasili na Utalii, Hamis Kigwangala ameteua wajumbe sita kwenye bodi hiyo walioteuliwa baada ya Rais John Magufuli kuongeza muda wa miaka mitatu kwa mwenyekiti wa bodi hiyo, Prof. Faustine Bee.
”Wote tunajua sekta ya utalii nchini imepata mtikisiko mkubwa kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa corona, kutokana na uzoefu tuliopata ni vyema bodi hii ikaelekeza chuo kuandaa mitaala mahususi itakayojielekeza zaidi kwenye matumizi ya teknolojia na usimamizi wa wanyamapori na utalii, ili majanga yanapojitokeza tuweze kukabiliana nayo,” amesema Kanyasu.
Kanyasu amemwagiza Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk. Aloyce Nzuki kukabidhi chuo hicho vitalu vilivyo wazi kwa ajili kukisaidia kutoa mafunzo kwa wataalam wa uwindaji wa utalii.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Aloyce Nzuki aliitaka bodi ya chuo hicho, kutengeneza kwa haraka utaratibu wa kutoa wataalam wa uwindaji wa utalii.
Amesema, baadhi ya waliopo kwa sasa ni wachache katika fani hiyo na kwamba hawakidhi mahitaji yaliyokusudiwa.
Leave a comment