WAKILI Tito Magoti, mtumishi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), anadaiwa kukamatwa na watu wasiojulikana, asubuhi ya leo tarehe 20 Desemba 2019. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa za kukamatwa kwa wakili huyo, zilianza kutolewa na Mwanaharakati Bob Chacha Wangwe, kupitia ukurasa wake wa Twitter.
Kwa mujibu wa Wangwe, Tito amekamatwa na watu watano waliovaa mavazi ya kiraia maeneo ya Mwenge jijini Dar es Salaam, ambapo walimuingiza kwa nguvu katika gari aina ya Harrier na kuondoka naye kusikojulikana.
MwanaHALISI ONLINE imemtafuta Anna Henga, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, kwa ajili ya ufafanuzi wa tukio hilo, ambapo amekiri kupokea taarifa hizo.
Henga amesema wamefikisha taarifa hizo kwenye Kituo cha Polisi cha Mburahati jijini Dar es Salaam, ambapo wameelezwa kwamba, Tito hashikiliwi kituoni hapo.
Kiongozi huyo wa LHRC amesema Polisi wameahidi kufanya uchunguzi wa tukio hilo.
“Tumeenda Kituo cha Polisi cha Mabatini ambacho ndio kituo kikubwa, wamesema hawana taarifa za kukamatwa Tito, bali watachunguza tukio hilo. Wametuambia na sisi tuendelee kumtafuta,” amesema Henga.
Mtandao huu ulimtafuta Kamanda Musa Taibu, Kamanda wa Jeshi la Polisi Kinondoni, kwa ajili ya kufahamu taarifa zaidi kuhusu kutekwa kwa mwanaharakati huyo, lakini jitihada hizo hazikufanikiwa.
Badala yake, alipokea mtu aliyejitambulisha kuwa ni msaidizi wake, na kueleza kwamba, Kamanda Taibu yuko msikitini, hivyo atafutwe baada ya swala.
Wakili Tito anayefahamika zaidi kama Mwanaharakati wa Haki za Binadamu, amekuwa akitumia ukurasa wake wa Twitter kuikosoa serikali.
Leave a comment