LEO mapema klabu ya Yanga ilimtangaza Zlatko Krmpotic ambaye ni raia wa Serbia mwenye umri wa miaka 62, kuja kukinoa kikosi hicho kwa mkataba wa miaka miwili kuanzia msimu huu wa mashindano 2020/21. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Licha ya Yanga kumpa mkataba wa miaka miwili lakini rekodi za hivi karibuni za kocha huyo hakuwahi kudumu ndani ya klabu yoyote kwa muda wa miaka hiyo miwili.
Ikumbukwe kocha huyo anakuja kuchukua nafasi ya Luc Eymael ambaye naye alidumu kwa miezi sita, ndani ya kikosi cha Yanga kabla ya uongozi wa timu hiyo kumtimua mara baada ya msimu wa 2019/20 kumalizika licha ya timu hiyo kumaliza katika nafasi ya pili kwenye msimamo.
Kocha huyo alianaza kazi hiyo 1 Julai, 1997 kwa kuanza kukinoa kikosi cha FC Shkupi na klabu ya mwisho kufundisha kabla kujiunga na Yanga ilikuwa Polokwane City inayoshiriki Ligi Kuu nchini Afrika Kusini.
Krmpotic alijiunga na Polokwane 18 Julai, 2019 na kukaa na timu hiyo kwa muda wa miezi mitatu na siku 10, kisha kutimuliwa baada ya kufungwa michezo mitano mfululizo.
Kabla ya hapo kocha huyo pia alifanikiwa kufundisha klabu ya APR ya Rwanda, ambapo aliajiliwa 8 Februari, 2020 ambapo alidumu ndani ya timu hiyo kwa muda wa siku 159 na baadae kutimka.
Krmpotic pia alifanikiwa kufundisha klabu ya Janeng Galaxy inayoshiriki Ligi Kuu nchini Botswana kuanzia 15 Januari, 2018 na kuhudumu ndani ya kikosi hiko kwa siku 189 na baadae kutimkia zake Royal Eagle.
Rekodi nyingine ya kushangaza ya Krmpotic ni kukaa ndani ya kikosi cha Zesco United ya nchini Zambia kwa muda wa siku 165, katika msimu wa 2017/18.
Pengine hali hiyo inaweza kuwa tofauti ndani ya klabu ya Yanga ambayo imeonekana kufanya usajili mkubwa kwa wachezaji wa ndani na nje ya nchi huku lengo kubwa ni kushinda taji la Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu 2020/21 unatarajia kuanza 6 septemba, 2020.
Kocha huyo anatarajia kuingia nchini siku ya kesho na kujiunga moja kwa moja na kikosi hicho ambacho kinatarajia kucheza mchezo wa kirafiki siku ya Jumapili 30 Agosti 2020 kwenye tamasha la kilele cha siku ya Mwananchi ambaye mgeni rasmi atakuwa Rais mstaafu wa awamu ya nne Dk. Jakaya Mrisho Kikwete
Leave a comment