BARAZA Kuu la Chama cha Demokrasia na Maendelea (Chadema) kimependekeza kwa mkutano mkuu wa chama hicho, Said Issa Mohamed kuwa mgombea Urais wa Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
Mapendekezo hayo yamefanywa na baraza hilo leo Jumatatu tarehe 3 Agosti 2020 katika mkutano unaofanyika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Mkutano mkuu wa chama hicho utakaofanyika kesho Jumanne, utathibitisha jina hilo la Mohamed ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chadema-Zanzibar.
Akizungumza na wajumbe wa mkutano huo, Mohamed amesema, “mtaniunga mkono na kwa mara ya kwanza, kijana mdogo kabisa anakuwa Rais ndani ya nchi ya Zanzibar na dunia itashangaa.”
“Katika mapambano na ujasili mnanifahamu vya kutosha. Tunasema sasa basi. Tumeamua kuweka mgombea urais Zanzibar ni kutekeleza lengo la chama kuwa na mgombea urais wa Zanzibar na kwa mara ya kwanza, tunakwenda kushinda,” amesema Mohamed
“Naweza, nitumeni, niko tayari kupeperusha bendera ya Chadema upande wa Zanzibar. Wanasema mzigo mzito mpe Mnyamwezi lakini mzigo wa hatari ili ufike mpe Mpenda,” amesema
Baada ya kumaliza kujinadi, Freeman Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema aliwauliza wanaokubali pendekezo hilo walikubali huko watano wakipinga.
Mbowe amesema, Said Issa Mohamed amependekezwa kwenda mkutano mkuu.
Mohamed anakwenda kuchukuana na wagombea wengine akiwamo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Hussein Ali Mwinyi aliyepitishwa kuwania urais.
Leave a comment