SIMBA wamefanikiwa kutwaa Ngao ya Jamii kwa mara ya pili mfululizo baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mtibwa Sugar Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Hiyo inakuwa mara ya nne kwa Simba kutwaa Ngao ya Jamii, baada ya 2011 wakiifunga Yanga 2-0, 2012 wakiifunga Azam FC 3-2 na mwaka jana wakiwafunga tena mahasimu wao wa jadi, kwa penalti 5-4 baada ya sare ya 0-0.
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Elly Sasii aliyesaidiwa na Hellen Mduma wote wa Dar es Salaam, na Ferdinand Chacha wa Mwanza, hadi mapumziko Simba walikuwa mbele kwa mabao 2-1.
Mshambuliaji Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda, Meddie Kagere alianza kuifungia Simba dakika ya 29 kwa shuti kali kutokea pembezoni mwa Uwanja kushoto, baada ya kuwatoka mabeki wa Mtibwa Sugar na kipa wao, Benedictor Tinocco kufuatia kazi nzuri ya Hassan Dilunga.
Kelvin Sabato akaisawazishia Mtibwa Sugar dakika ya 33 baada kupokea pasi nzuri ya Saleh Hamisi na kufumua shuti zuri akiwa anatazamwa na mabeki wa Simba.
Wakati refa Sasii anajiandaa kupuliza filimbi ya kukamilisha kipindi cha kwanza, Hassan Dilunga akaifungia Simba bao la pili dakika ya tatu ya muda wa nyongeza baada ya dakika 45 stahili za mchezo.
Dilunga aliyesajiliwa kutoka Mtibwa Sugar mwezi uliopita tu baada ya awali kuchezea Ruvu Shooting, Yanga na JKT Ruvu, alifunga bao hilo kwa shuti lililowababatiza wachezaji wengine kufuatia pasi ya Mganda, Emmanuel Okwi.
Kipindi cha pili mchezo uliendelea kupendeza, Simba wakisaka mabao zaidi na Mtibwa Sugar wakitafuta bao la kusawazisha lakini hakuna timu iliyofanikiwa kutikisa nyavu.
Mtibwa ilipata pigo baada ya kiungo wake, Awadh Juma kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake imechukuliwa na Juma Luizio dakika ya 63, wote wamewahi kuchezea Simba.
Nahodha wa leo wa Simba, Emmanuel Okwi naye akashindwa kuendelea na mchezo dakika ya 66 akimpisha Nahodha wa klabu, John Bocco.
Leave a comment