RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Maguful ametoa pole kwa familia ya Balozi Mstaafu Job Lusinde aliyefariki dunia tarehe 07 Julai, 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa imesema, Rais Magufuli amekwenda msibani kwa Balozi Lusinde nyumbani kwake Kilimani Jijini Dodoma leo Alhamisi tarehe 9 Julai 2020.
Rais Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amekwenda nyumbani hapo akitokea Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Jijini Dodoma ambako ameongoza Kikao cha Kamati ya Maadili na Usalama na Kikao cha Kamati Kuu ya CCM.
Akiwa nyumbani kwa Marehemu Balozi Mstaafu Lusinde, Rais Magufuli amekutana na Mjane wa Marehemu, Sara Lusinde, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu ambapo ameeleza kuguswa na kifo cha Balozi Mstaafu Lusinde.
Amesema, daima atamkumbuka kwa mchango wake alioutoa akiwa waziri wa ujenzi, ushauri wake mzuri na moyo wake wa upendo na ukweli.
Rais Magufuli ameeleza wakati wa utumishi wake, Balozi Mstaafu Lusinde alikuwa mzalendo wa kweli, mchapakazi na aliyetetea maslahi ya Tanzania na kwamba hata alipostaafu aliisemea vizuri Dodoma.
Amewataka wafiwa wote kuwa wastahimilivu na kumpuzisha salama hapo kesho Ijumaa tarehe 10 Julai, 2020 atakapozikwa.
Leave a comment