WAKATI hofu juu ya usalama wa maisha ya wananchi wa Kibiti, Pwani ikizidi kutanda baada ya tukio la mauaji ya askari Polisi nane yaliyotekelezwa na watu wasiojulikana juzi, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mwigulu Nchemba amelivalia njuga sakata hilo, anaandika Hamisi Mguta.
Askari hao walikuwa wakiingia katika kituo cha kazi juzi majira ya 12 Jioni ndipo waliposhambuliwa na risasi na majambazi katikaa kijiji cha Mkengeni wilaya Rufiji mkoani humo.
Watu hao wasiofahamika walimshambulia dereva wa gari la Polisi namba PT. 3713 Toyota L/Cruiser (Pickup) lililokua limebeba jumla ya askari tisa na kupelekea gari hilo kupoteza muelekeo na kunasa pembeni ya barabara ambapo walipata nafasi ya kuwamalizia wengine waliokuwa wakijitahidi kutoka na kujitetea kwa kuwatiririshia risasi, huku askari mmoja akifanikiwa kukimbia.
Akiwa mkoani humo katika maombolezo ya kuaga miili ya askari hao, Waziri Mwigulu amesema watahakikisha wanawatafuta waliohusika na mauaji hayo.
“Kama wamewashambulia ili waone kitakachofuata sisi tutawaonesha kitakachofuata, na hiki kilichofanyika ni hatua ya mwisho, wananchi waliowema katika maeneo yale wajue kwamba serikali katika viapo vya vijana wake tutawalinda kwa ghalama zozote kuhakikisha usalama wa maisha yao yapo,” amesema.
Mwigulu ambaye aliongozana na Naibu wake Eng. Hamad Masauni amesemea kuwa waliotekeleza mauaji hayo pamoja na wanaoshirikiana nao wote watakua kwenye kundi moja kuhusishwa na mauaji hayo hivyo watatafutwa popote walipo hata kama wakiwa wamejificha kwenye nyasi.
“Hawa waliofanya hivi kama watajificha kwenye nyasi, hatutabakisha hata unyasi uliosimama wao wapate nafasi ya kujificha na wale wanaoshirikiana nao watakua sehemu ya wahalifu wanaoshiriki,
“Tukimaliza kuaga askari wetu hapa naomba viongozi tukae pembeni kugawana majukumu hatuwezi kukubali hali hii,” amesema.
Aidha Mwigulu amewaambia wananchi kuwa hakuna anayepewa nafasi ya kuogopa na lazima mtu achague kuunga mkono upande mmoja iwe kati ya serikali au wahalifu.
“Tuliwaambia wakati ule na sasa hivi tunasema hakuna kuwa katikati, hapa ni ama upo na serikali ama upo na wahalifu,” amesema.
Ikumbukwe kuwa mauaji katika Wilaya ya Kibiti yamewahi kutokea miaka kadhaa iliyopita iliyowahusisha polisi zaidi ya 10, wenyeviti na viongozi mbalimbali wa vijiji suala ambalo halijapata kujulikana sababu za mauaji hayo kutokea wilayani humo.
Leave a comment