BALOZI za Marekani na Uingereza nchini Tanzania wameingilia kati sakata la kukamatwa mwandishi wa habari za uchunguzi, Erick Kabendera. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Leo tarehe 9 Agosti 2019 balozi hizo zimetoa tamko kuhusu tukio hilo, zikieleza kwamba ni muendelezo wa matukio ya watu kutiwa kizuizini kwa muda bila kupelekwa mahakamani na kubadilishiwa mashitaka na mamlaka za sheria nchini.
Kupitia tamko hilo la pamoja balozi hizo zimeeleza kuwa, matukio hayo yanazidi kuleta wasiwasi sambamba na kuzorotesha mchakato wa haki za raia na kisheria nchini Tanzania .
“Tuna wasiwasi hasa kwa tukio la hivi karibuni jinsi ambavyo halikushughulikiwa kwa haki la kukamatwa, kuwekwa kizuizini na tuhuma za mashitaka ya mwandishi wa habari za kiuchunguzi, Erick Kabendera,” inaeleza sehemu ya tamko la balozi hizo.
Tamko hilo limeeleza kwamba, Kabendera alinyimwa haki ya kuwa na mwanasheria katika hatua za awali za kutiwa kizuizini, huku likidai kuwa ni kinyume na sheria ya makosa ya jinai.
“Ikizingatiwa ukweli kwamba alinyimwa haki ya kuwa na mwanasheria kwenye hatua za awali za kutiwa kizuizini ambapo ni kinyume na Sheria ya Makosa ya Jinai,” inaeleza tamko hilo.
Balozi hizo zimeisihi Serikali ya Tanzania kutoa hakikisho la mchakato wa kutenda haki kisheria kwa raia wake, kama ilivyotambua haki ya msingi ya kuridhia kwenye mikataba mbalimbali ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa, ikiwemo Azimio la Kimataifa la Haki za Raia na Kisiasa.
Kabendera anayekabiliwa na mashtaka matatu likiwemo uhujumu uchumi, utakatishaji fedha kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, yuko mahabusu ya Gereza la Segerea jijini Dar es Salaam, baada ya kukosa dhamana katika kesi inayomkabili.
Mwandishi huyo alipandishwa kizimbani tarehe 5 Agosti mwaka huu, ikiwa ni siku saba zimepita tangu alipokamatwa na maafisa wa Jeshi la Polisi tarehe 29 Julai 2019.
Awali, Idara ya Uhamiaji nchini Tanzania ilithibitisha kwamba ilishirikiana na Jeshi la Polisi kumkamata Kabendera kwa ajili ya kumhoji kuhusu utata wa uraia wake.
Lakini baadae, Kabendera alipandishwa kizimbani na kusomewa mashitaka matatu, ikiwemo ya kujihusisha na mtandao wa uhalifu (uhujumu uchumi), kukwepa kodi kiasi cha Sh. 173.2 na utakatishaji fedha, makosa anayodaiwa kutenda kuanzia mwaka 2015 hadi 2019.
Leave a comment