SERIKALI ya Kenya imewazuia madareva 25 wakiwamo 23 wa Tanzania kuingia nchini humo baada ya kuwapima na kuwakuta na maambukizo ya virufi vya corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Madereva wengine wawili, mmoja anatoka Uganda na mwingine wa Rwanda.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano tarehe 13 Mei 2020, naibu waziri wa Afya, Dk Rashid Aman amesema madereva hao walipimwa katika kipindi cha saa 24 na kukutwa na maambukizo ya COVID-19.
Wizara hiyo imesema kwamba hatua hiyo inalenga kuwalinda Wakenya dhidi ya maambukizi kutoka kwa raia wa kigeni.
Amesema katika mapambano ya COVID-19, wanatarajia kuanzisha maabara mbili za kuhama ili kuongeza upimaji zitakazowekwa mpaka wa Namanga.
Dk Aman amewataka Wakenya kuchukua tahadhari na kuwaripoti watu ambao wanawashuku kuingia nchini humo kwa njia za panya.
Katika maelezo yake, Dk Aman amesema wagonjwa wapya 22 wameripotiwa nchini humo hivyo kwa sasa Taifa hilo idadi ya wagonjwa wa Covid-19 wamefikia 737.
Dk Aman amesema idadi hiyo inatokana na watu 1,516 waliopimwa katika muda wa saa 24 zilizopita.
Amesema mpaka sasa, Kenya imefanikiwa kuwapima watu 35, 432.
Leave a comment