RAIS Mstaafu wa awamu ya nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete atakuwa mgeni rasmi kwenye tamasha la klabu ya Yanga maarufu ‘Siku ya Mwananchi’ litakalofanyika Jumapili tarehe 30 Agosti, 2020 Uwanja wa Mkapa Jijini Dar es Salaam. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya uwepo wake kwenye tamasha hilo imetolewa na klabu ya Yanga kupitia kurasa mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii ya Facebook, Twitter na Instagram.
Mstaafu huyo ambaye ni shabiki wa klabu hiyo ataungana na mashabiki wengine wa Yanga siku ya Jumapili, ambapo watatambulishwa wachezaji watakaoenda kuitumikia timu hiyo katika msimu ujao wa mshindano unaoanza tarehe 6 septemba, 2020.
Katika tamasha hilo, Yanga itacheza mchezo wa kirafiki na klabu ya Aigle Noir kutoka Burundi ambayo inatarajiwa kufika nchini kesho Ijumaa.
Shauku kubwa ya mashabiki na wapenzi wa klabu hiyo ni kuona wachezaji wapya waliosajiliwa katika dirisha kubwa la usajili ambao linatarajiwa kufungwa tarehe 31 Agosti, 2020.
Mpaka sasa Yanga imeshajiri wachezaji 11 kutoka ndani na nje ya Tanzania ambao watatumika kwenye msimu ujao wa 2020/21.
Viingilio kwenye tamasha hilo vitakuwa Tsh. 5,000 kwa mzunguko, Tsh. 20,000 kwa VIP B na C na Tsh. 30,000 kwa upande wa VIP A.
Leave a comment