MFUKO wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) umejipanga kutumia mfumo wa kielektroniki katika kuhakiki na kuzipata kaya maskini kwenye kipindi cha pili ya mpango wa kunusuru kaya maskini wa TASAF III ili kuondokana na kuingiza wasio maskini katika mpango huo na kuwapata walengwa sahihi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Mkurugenzi wa TASAF, Ladislaus Mwamanga alisema hayo mjini Morogoro katika kikao kazi baina ya wahariri wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari nchini na TASAF.
Aidha alisema mfumo huo katika utawafanya kubaini watu ambao hawana sifa pamoja na wale ambao wameshafariki dunia na kuwaondoa kwenye kunufaika na mpango huo.
Mwamanga alisema TASAF awamu ya tatu kipindi cha pili itatumia kiasi cha shilingi trilioni 2 kwa kipindi cha miaka minne ambapo itazifikia Halmashauri na wilaya 185 Tanzania Bara na Visiwani.
“Katika awamu ya tatu kipindi cha kwanza utekelezaji wake ulifanikiwa kwa asilimia 70, na zilitumika shilingi trilioni 1.7 kwa miaka saba na sasa tunaendelea kuhawilisha,” alisema.
Hata hivyo alisema zaidi ya kaya 1,320 zilijitoa zenyewe baada ya kuona zinajitosheleza kiuwezo kufuatia kupokea fedha za uhawilishaji katika kipindi cha TASAF II na III awamu ya kwanza.
Kwa upande wake katibu tawala mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emannuel Kalobero aliwahimiza waandishi wa habari, kuelimisha wananchi hususani walengwa wa mpango wa kunusuru kaya maskini kutumia vyema fursa hiyo adhimu iliyowekwa na serikali kupitia TASAF ili kasi ya kupambana na umaskini iendelee kuwa na mafanikio.
Alisema kwa kiasi fulani inaweza kusemwa mpango huo wa TASAF umesaidia kuinua uchumi wa nchi na kufikia uchumi wa kati kufuatia walengwa wengi kufikiwa ambao wamezitumia fedha zao katika kuanzisha miradi mbali na kujitegemea kiuchumi.
Pia alisema elimu hiyo isaidie kutoa nafasi kwa wale waliofanya vizuri kujiondoa kwenye mpango kwani mpango huo na kuwa kichocheo kwa wengine kuondoka na kupisha wenzao na kutambua kuwa sio kwamba wanatakiwa kuwem kwenye mpango kwa miaka yote.
Leave a comment