Saturday , 27 April 2024
Home Habari Mchanganyiko Rais Magufuli apingwa
Habari Mchanganyiko

Rais Magufuli apingwa

Dk. John Pombe Magufuli, Rais wa Tanzania
Spread the love

MSIMAMO wa Rais John Magufuli kuhusu katazo la watakaopata mimba katika utawala wake kutopata haki ya kurudi shuleni imeibua mjadala mpana mitandaoni, sehemu kubwa ya wachangiaji wakipingana na rais, anaandika Pendo Omary.

Rais Magufuli alitoa kauli hiyo mjini Bagamoyo jana jioni wakati wa ziara yake ya siku tatu mkoani Pwani ambako alizindua viwanda saba na barabara ya Bagamoyo-Msata ya kilometa 64 iliyogharimu Sh. 183 Bilioni.

“Serikali inatoa mabilioni ya hela kwa ajili ya elimu bure, halafu zinakuja NGOs zinasema eti anayepata mimba akishazaa aruhusiwe kurudi shuleni… hizi NGOs zikafungue shule za wazazi siyo zilazimishe serikali kusomesha wazazi. Mwisho utakuta darasa la kwanza wote wanawahi kwenda kunyonyesha,” alisema Rais Magufuli.

Wakichangia baada ya tamko la Rais, Vicessia Shule, Mwalimu wa sanaa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika ukurasa wake wa Facebook, ameandika: “Nimegundua hii ni vita, them against us (wao dhidi yetu). Vita ni vita! Tukilegea watatumaliza. Tunajua watoto wetu wanayo haki ya kupata elimu bila ya kujali vikwazo vinavyotokana na maumbile yao).

“Nimeshasema hamna kulaliwa, lazima tuwalalie wao, tumelaliwa mno, tumechoka kulaliwa, iwe zamu yetu sasa kuwalalia wao… Ukitaka tuunge mkono harakati za makinikia na Ikwiriri ni lazima twende pamoja kwenye ajenda yetu ya ukombozi wa wanawake kimapinduzi. Ni lazima tusimame kwenye misingi ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Ilani yenu ya uchaguzi.

“Wanawake ni takribani asilimia 52 ya idadi ya Watanzania wote. Huwezi kuwapuuza, huwezi kuwadhalilisha, huwezi kuwadharau na ukafanikiwa. Haiwezekani,” ameandika Dk. Shule.

Mwanaharakati wa masuala ya elimu, Demere Kitunga ameandika: “Habari ya kuadhibu watoto kwa ‘mmomonyoko wa maadili’ walioanzisha wazee wao, kwa hulka ya kimaumbile walionyimwa nyenzo za kukabiliana nazo, kwa kuingia kwenye mitego iliyosheheni katika mazingira wanamokulia, kwa kuwa na maumbile yanayokomaa kabla ya ukomavu wa akili nk, nk. si sahihi kabisa. Tujadili jinsi gani ya kukabiliana na maono ya namna hii.”

Richard Mabala, Mwalimu, mwandishi wa vitabu vya kufundishia shule za msingi na sekondari na mwanaharakati wa haki za binadamu, akijadili suala hilo, naye ameandika: “Naomba nieleweshwe mpango wa serikali na wa jamii kuwalinda wasichana wetu wakienda na kutoka shuleni, wakiwa shuleni, wakipanda daladala, wakienda sokoni n.k.

“Maana hawako salama mahali popote (rejea tafiti za TAMASHA na wengine). Ukiwauliza wasichana wanatongozwa mara ngapi kwa siku kuanzia wakiwa na miaka 13 hivi, kwa walio wengi si chini ya mara 5-10 kwa siku!!! Viherehere vya wanaume vitatumaliza.”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Wakili: Ukimpa zawadi mwenza marufuku kumpora hata mkiachana

Spread the love  WANANDOA na watu waliko kwenye mahusiano ya kimapenzi, wamekumbushwa...

Habari Mchanganyiko

Majaliwa: Mvua zimesababisha vifo vya watu 155, kuendelea hadi Mei

Spread the love  WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema mvua kubwa za El-Nino...

Habari Mchanganyiko

Exim Bank yatoa  vitanda kwa shule ya Jeshi la Polisi Moshi

Spread the love  BENKI ya Exim imekabidhii  seti ya vitanda kwa Shule...

Habari Mchanganyiko

NBC yakabidhi vitanda Shule ya Polisi Moshi

Spread the loveBenki ya NBC imekabidhi msaada wa vitanda 28 kwa Shule...

error: Content is protected !!