Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amewataka Wajumbe wa Sekretarieti ya Kamati Maalum ya NEC- CCM Taifa Zanzibar waliopitisha pendekezo kumtaka aridhie kuongeza muda wa urais Visiwani humo, kufunga mjadala huo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Jana Jumapili Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dk. Mohamed Said Dimwa, alisema wajumbe hao wamepitisha pendekezo la kuishauri Kamati Maalum ya NEC kuridhia kuongeza muda wa Rais Dk. Mwinyi kuongoza nchi katika muhula wake wa kwanza kwa kipindi cha miaka saba badala ya mitano.
Maoni hayo yalikwenda mbali zaidi hata kutaka Uchaguzi Mkuu wa mwakani kumchagua Rais wa Zanzibar usifanyike.
Katika taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Mkurugenzi wa Mawasiliano, Ikulu Zanzibar, Charles Hilary imesema jambo hilo halina tija wala faida kwa nchi na CCM yenye kufuata misingi ya demokrasia.
“Rais Dk. Mwinyi ni muumini wa kufuata Katiba na Sheria za nchi, tunapenda kusisitiza kwamba maoni haya si ya Rais wala sio ya Chama Cha Mapinduzi Zanzibar.
“Kwa muktadha huu, Rais Dk. Mwinyi ataendelea kuheshimu utaratibu uliowekwa wa Rais kuchaguliwa kila baada ya miaka mitano. Aidha, amewasihi wale wote wenye mawazo tofauti na hayo wafunge mjadala huo,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment