Mwanaharakati Godlisten Malisa, ametiwa mbaroni na askari wa jeshi la Polisi muda mchache baada ya kutoka kwenye chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu walipofika kwa ajili ya usikilizaji wa shauri namba 11805 la mwaka 2024 linalomkabili. Anaripoti Faki Sosi …(endelea).
Malisa na Meya Mstaafu wa Ubungo, Boniface Jocob (Boniyai) wanakabiliwa na shauri la kuchapisha taarifa za uongo kwenye mtandao.
Malisa na Boniyai walifika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo tarehe 6 Juni 2024 mbele Hakimu Mkazi Mkuu Ushindi Swallo kwa ajili ya usikilizaji wa awali wa kesi yao .
Wakili wa serikali Happy Mwakanyamale alidai mahakamani hapo kuwa upande wa Mashtaka hautaweza kuwasilisha hoja za awali kwa kuwa mshtakiwa namba mbili hayupo mahakamani.
Mshtakiwa namba mbili kwenye shauri hilo ni Malisa ambaye alichelewa kufika mahakamani hapo.
Hakimu Swallo aliahirisha kesi hiyo mpaka tarehe 4 Julai 2024 na kusema kuwa kitendo cha mshtakiwa Malisa kuchelewa kufika kwenye shauri hilo kutasababisha kufutiwa kwa dhamana yake.
Malisa alifika mbele ya hakimu Swallo kabla hajatoka kwenye chumba cha mahakama na kujisalimisha kwa Hakimu aliyemhoji sababu ya kuchelewa ambapo Malisa alimuomba radhi na kumueleza kuwa alichelewa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo anauguza.
Baada ya maelezo hayo Hakimu Swallo alimuonya kuwa akirudia kitendo hicho atamfutia dhamana.
Hatua hiyo imepelekea mahakama kutofuta dhamana ya Malisa lakini baada ya kutoka kwenye chumba cha mahakama askari wa jeshi la Polisi walimkamata Malisa na kumpeleka mahabusu.
Mmoja mawakili wanaowawakilisha Malisa na ‘Boniyai’ amesema kuwa mteja wake yupo mikononi mwa Jeshi la Polisi na huenda akasafirishwa kupelekwa mkoani Kilimanjaro.
Leave a comment