WAZIRI wa Nishati nchini Tanzania, January Makamba amesema, Serikali itaendelea kutumia vifaa mbalimbali vya umeme vinavyozalishwa nchini hivyo, wazalishaji wanapaswa kuzingatia ubora wanapovizalisha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Waziri Makamba alisema hayo jana Jumanne, tarehe 14 Desemba 2021, mara baada ya kutembelea Kiwanda cha Africab, jijini Dar es Salaam, kuangalia shughuli za uzalishaji wa vifaa vya umeme na mikakati yao.
Alisema, Serikali kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA), “tupo katika kuharakisha usambazaji wa umeme vijijini kupitia REA. Sasa ziara hii yangu ni kuangalia shughuli za uzalishaji wa nyaya za kusambaza na vifaa mbalimbali vya umeme, kuangalia uwezo wa kiwanda, kuangalia mipango yao ya upanuzi.”
Makamba ambaye kwenye ziara hiyo aliongozana na naibu wake, Stephen Byabato alisema, wanafarikija kuona wazalishaji wa vifaa hivyo wa ndani wanaofanya shughuli hizo kwa ubora na Serikali itaendelea kuwaunga mkono.
“Kutakuwa na mahitaji makubwa sana ya nyaya, kwani katika maeneo ambayo umeme haujafia kwa wananchi ili ufike zinahitajika kilomita 120,200 za nyaya za umeme mdogo.”
“Nyaza za umeme wa kati zinatakiwa kilomita 110,000 hivi, ukijumulisha zinatakiwa kama kilomita 340, 000 za nyaya za umeme ili kufikisha katika vitongoji vyote 37,000 ambavyo havijapata umeme,” alisema Makamba
“Tunatakiwa kuwa na transfoma 38,000 na kwa mahitaji hayo tunatarajia kuwafikia watumiaji kama milioni tatu kwa miaka ya karibuni, ni kazi kubwa, inahitaji vifaa vingi,” alisisitiza
Aidha, Waziri Makamba aliupongeza uongozi wa kiwanda hicho kwa uwekezaji wao mkubwa na kuwasisitiza, bidhaa wanazozalisha sharti ziwe na viwango.
Kwa upande wake, Ofisa Masoko wa Kampuni ya Africab, David Tarimo alimshukuru Waziri Makamba na Naibu wake, Byabato kwa kuwatembelea na kuahidi kutekeleza maagizo waliyoyatoa.
“Tumefarijika kwa kututembelea kuona uzalishaji na kile tunachokifanya. Hii inaonesha wazalishaji wa ndani kama tukipewa fursa tunaweza kulijenga Taifa letu,” alisema
Alisema wanapanua kiwanda hicho kwa kujenga kingine eneo la Kimbiji mkoani Pwani.
Leave a comment