KATIBU Tawala Wilaya ya Kinondoni, Stella Msofe amezindua Kitabu cha ‘Jinsi ya Kumpata Mpezi Bora wa Maisha’ kilichotungwa na Mchungaji wa Kanisa la Power of God Fire, Justine Kipeta. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kinondoni … (endelea).
Sherehe za uzinduzi wa kitabu hicho, zilifanyika Jumapili tarehe 31 Agosti 2020, katika kanisa hilo wakati wa ibada ambapo Msofe alimpongeza Kipeta kwa kuandika kitabu hicho.
“Tukiwa na taasisi njema ya ndoa, tunapata wale watu wanaohitajika ikiwemo kupata kizazi kilicho bora kinachofuata maadili bora, siyo tu ya kanisani bali hata kanuni, taratibu na sheria za nchi.”
“Kuna mmomonyoko wa maadili duniani, sasa hivi tunatumia simu zetu na zinatufundisha mambo mengi sana, hivyo tutumie mitandao ya kijamii katika kujifunza yale yaliyo mema katika tamaduni zetu za Kitanzania,” alisema Msofe.
Danton Rweikila, askofu wa kanisa hilo amesema, kitabu hicho kimewalenga vijana wanaopitia katika mahusiano hususani kijana kumpata mwenza bora atakayeweza kuishi naye katika maadili ya Kimungu.
“Vijana wanaingia mahusiano wakiwa na umri mdogo hivyo wanapokuwa wazazi, wanakuwa hawana uwezo wa kuwalea watoto wao kwa kukosa muda wa kukaa nao kutokana na changamoto za maisha.”
“Vijana wanapokuja kanisani, wanapewa semina ya maisha yao hasa wanapoingia kwenye mahusiano ya ndoa,” amesema Rweikila.
Mchungaji Justine Kipeta, mwandishi wa kitabu hicho amesema, kitabu hicho kitasomwa na watu wa rika zote na watakaposoma kitawatoa sehemu moja na kwenda sehemu nyingine.
Kipeta amesema, kwenye kitabu hicho mada zipo saba ikiwemo kwa nini vijana wengi huingia kwenye mahusiano mabovu na kujikuta wakiingia kwenye ndoa tata.
“Utakuta mwingine anasema eti kabla ya kuoana uanze kuwa na mahusiano halafu baadaye muoane, hiyo ni hatari sana. Kinachotakiwa umuombe Mungu ili upate mtu sahihi kwao,”amesema Kipeta.
Leave a comment