Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba amependekeza kutoza ushuru wa bidhaa kwa kiwango cha asilimia 10 kwenye thamani ya dau la kamari kwenye michezo ya kubahatisha na Bahati Nasibu ya Taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Amesema mapato yatakayokusanywa kutoka chanzo hiki ni kwa ajili ya kugharamia bima ya afya kwa watu wasio na uwezo na makundi maalum hususan wanawake wajawazito na watoto wa umri chini ya miaka mitano.
Akiwasilisha bungeni jijini Dodoma leo Alhamisi mapendekezo ya serikali kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2024/2025, amesema hatua hiyo inatarajia kupeleka kiasi cha Sh. 29.5 bilioni kwenye mfuko mkuu wa serikali.
Pia amependekeza kutoza ushuru wa bidhaa kwa kiwango cha asilimia 10 kwenye ada ya matangazo ya biashara za Michezo ya Kubahatisha na Bahati Nasibu ya Taifa yanayotangazwa kupitia vituo vya televisheni, redio, na tasnia ya uchapishaji.
“Lengo la hatua hii ni kuongeza wigo wa kodi. Hatua hii inatarajia kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi milioni 9,150,” amesema.
Leave a comment