JAJI Eliezer Feleshi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) nchini Tanzania, amesema wanahabari wanapaswa kuwa na bodi watayoisimamia wenyewe kulinda maadili ya habari. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Amesema, chombo hicho ndio kitachokuwa na wajibu wa kusimamia wanahabari na hata kuwashughulikia endapo watakwenda kinyume na maadili ya habari.
Jaja Feleshi ametoa kauli hiyo leo Jumatatu tarehe 13 Juni 2022, ofisini kwake bungeni jijini Dodoma alipokutana na wadau wa habari.
“Sina tatizo, naona muwe na ‘regulator’, bodi yenu moja, ili mmoja wenu akienda kinyume na maadili (ya uandishi wa habari), mnamshughulikia nyinyi wenyewe,” amesema Jaji Eliezer Feleshi.
Jaji Feleshi ametoa kauli hiyo baada ya Deodatus Balile, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), kumweleza wanahabari wanapendekeza kuundwa kwa chombo kimoja kitakachosimamia wanahabari badala ya vyombo vinne kama inavyoelekezwa na sheria ya sasa.
Pia, Balile amemweleza Jaji Feleshi, miongoni mwa mambo yanayotisha wanahabari katika sheria iliyopo sasa, anaweza kufungwa bila hata ya yeye (mwanahabari) kuitwa kusikiliza kesi yake.
Jaji Feleshi amesema, sheria yoyote lazima ipitiwe vizuri na iwe na uhalali lakini pia iwe ya wananchi.
Mwanasheria huyo amesema, ofisi yake ipo pamoja na hatua zinazochukuliwa na wanahabari katika kuyaendea mabadiliko yanayotakiwa.
“Niko na nyinyi na Mheshimiwa Rais (Samia Suluhu Hassan) katika hatua kuelekea mabadiliko ya sheria za habari,” amesema.
Leave a comment