WABUNGE wa Bunge la Kenya wamelazimika kukimbia ofisi zao zilizoko Bunge Towers baada ya waandamanaji wanaopinga ushuru kwenye Muswada wa Fedha 2024, kuvamia majengo ya Bunge la nchi hiyo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa… (endelea).
Hata hivyo, tayari muswada huo unaolenga kuiwezesha Serikali ya Kenya kukusanya Ksh 347 bilioni (Sh trilioni saba), umepitishwa na baada ya wabunge 195 kupiga kura ya NDIO kuunga mkono muswada huo ulivyofanyiwa marekebisho huku wabunge 106 wakiupinga.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka vyanzo mbalimbali nchini Kenya, imeeleza waandamanaji nane wanadaiwa kupoteza maisha baada ya polisi kutumia risasi kuwasambaratisha waandamanaji hao.
Waandamanaji hao waliojawa na hamaki walivunja geti la uani la Bunge kupitia upande wa Uhuru Highway, kisha kuingia ndani na kuvunja vyoo na kufanya uharibifu pamoja na kula vyakula vya wabunge.
Maafisa wa polisi ambao wengi wao walionekana kulemewa na wingi wa waandamanaji hao walibaki kuwaangalia wasijue la kufanya huku vijana wakiingia kila upande mithili ya nyuki.
Waandamanaji hao waliingia ndani ya Bunge saa chache baada ya polisi kuwapiga risasi waandamanaji kadhaa nje ya Majengo ya Bunge.
Waandamanaji hao pia walichoma magari ya Polisi huku hali ya wasiwasi ikiongezeka nje ya bunge.
Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Kenya kwa waandamanaji kuvunja vizuizi na kuingia ndani ya Bunge licha ya ulinzi mkali.
Leave a comment