Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amewathibitishia wafanyabiashara waliofungua maduka leo Jumatatu licha ya kuwepo kwa mgomo kwa baadhi yao, kwamba atakayejaribu kuwafanyia vurugu atamuonesha ‘show’. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
“Yule atakayemletea mkwara aliyekubali kufungua, naapa mbele ya Mwenyezi Mungu, hapo ndipo nitakapoonyesha ‘show’ nzima. Kwa sababu mtu anakubali kufungua na wewe unamchimba mkwara, mimi ntakuchimba mkwara na hautainuka tena,” amesema.
Akizungumza na baadhi ya wafanyabiashara hao leo Jumatatu, Chalamila amesema pamoja na uwepo kwa mgomo wa baadhi ya wafanyabishara, atalinda biashara zao na hawatafanyiwa vurugu.
![](https://mwanahalisionline.com/wp-content/uploads/2024/06/e45f640b-5521-42e0-b6ac-a4761c892600.jpeg)
Pamoja na mambo mengine, Chalamila amesema kero zilizopelekwa na wafanyabiashara hao serikalini zinaendelea kushughulikiwa.
Naye Naibu Spika wa Bunge, Mussa Azzan Zungu amelieleza Bunge kwamba tayari kamati ya wafanyabiashara hao inakutana na serikali hivyo, wabunge waliotaka kauli ya serikali kuhusu sakata hilo akiwamo Mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Msukuma (CCM) kuwa wawe na subira.
Wafanyabiashara hao wamegoma kuishinikiza Serikali kutatua changamoto zinazowakabili, ikiwemo kamatakamata inayofanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Mgomo huo umeibuka baada ya juzi Jumamosi kusambaa vipeperushi kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuwepo kwa mgomo huo utakaoanza leo.
Hivi tukijiuliza tatizo ni nini hapo karihakoo? Utendaji, ufahamu, uelewa..! Kutoelewana au joto ya uchanguzi ujao?