SERIKALI imesema wananchi waliokwisha kuandikwa na kutambuliwa kwenye mfumo wa Kitambulisho cha Taifa, watapatiwa vitambulisho vyao ifikapo Machi 2024. Anaripoti Isaya Temu, TUDARCo… (endelea).
Hayo yamesemwa leo tarehe 8 Septemba 2023, bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Jumanne Sagini, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Sikonge, Joseph Kakunda.
Kakunda alihoji ni lini Serikali itamaliza kazi ya kuwapatia Wananchi Vitambulisho vya Taifa?
Akijibu swali hilo, Naibu waziri ameeleza kuwa kazi ya kuwapatia wananchi vitambulisho ni endelevu kwani Serikali inatambua uhitaji ni mkubwa, kuna wanaoharibu au kupoteza vitambulisho, wananchi wanaotimiza miaka kumi na nane na ambao walisajiliwa na hawakupata kitambulisho.
“Kwa wananchi ambao walitambuliwa lakini hawajapata vitambulisho vyao, Serikali inatarajia kuwapatia vitambulisho vyao ifikapo mwezi Machi 2024,” amesema.
Aidha, mbunge huyo alihoji swali la kwamba Serikali ina uhakika gani wa kutekeleza ahadi hiyo kwa kipindi cha miezi sita pekee wakati imeshindwa awali kutekeleza kwa muda wa miaka 14?
Akijibu swali hilo, Sagini amesema ana uhakika kwani kilichokuwa kinakwamisha shughuli hiyo ni mkataba kuvurugwa na mkandarasi aliyekuwa na madai ya muda mrefu.
“Hivyo kwa sasa Serikali imeshalipa madeni yote yaliyokuwa yakidaiwa na uzalishaji wa vitambulisho umeanza na yeye ameshakwenda kwenye kiwanda na ameridhishwa na uzalishaji uanaoendelea.
“Ofisi hiyo imepanua uwezo wake kwa kuazima hata wafanyakazi kutoka kwenye vyombo vyetu vingine vya usalama ili kuongeza kasi ya kuwafikia wananchi ili waweze kupata zile namba za utambulisho, kwa hivyo kuliko kusitisha zoezi lile ngoja liendelee ili wananchi (Sikonge) ambao hawajapata vitambulisho wapate,” amesema.
Leave a comment