SHEREHE ya Sikukuu ya Pasaka sasa itafanyika tofauti, ni baada ya Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, kupika marufuku sehemu za mikusanyika zilizozoeleka. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa SACP, Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Jeshi la Polisi katika kanda hiyo, mikusanyiko hiyo ikiwemo kwenda ufukweni na baa ni haramu katika kipindi hichi cha tishio la virusi vya corona (COVID-19).
Akizungumzia na wanahabari leo tarehe 9 Aprili 2020, kuhusu maadhimisho ya siku kuu hiyo inayotarajiwa kufanyika tarehe 12 hadi 13 Aprili 2020, Kamanda Mambosasa amesema, polisi wamejipanga kudhibiti mikusanyiko isiyo ya lazima, ili kuunga mkono jitihada za serikali katika kupambana na mlipuko wa virusi vya corona.
“Kanda Maalumu imejipanga kutekeleza maelekezo ya serikali ya kudhibiti mikusanyiko isiyokuwa ya lazima, katika kipindi chote cha pasaka, ili kujikinga na maambukizi ya Virusi vya Corona,” amesema Kamanda Mambosasa.
Wakati huo huo, Kamanda Mambosasa amewataka madereva wa pikipiki (Bodaboda) na bajaji walioruhusiwa kuingia kati kati ya miji, kufuata sheria, ikiwemo kuvaa kofia ngumu.
Amesema, katika kipindi hicho, polisi wamejipanga kuimarisha ulinzi kwa kufanya doria kwa kutumia miguu, pikipiki, magari, mbwa na farasi.
Leave a comment