WAKATI Serikali ya mkoa wa Dar es Salaam, ikiagiza watendaji wa Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka (Udart) kutoa sababu za kutochukua hatua madhubuti kuondoa kero ya usafiri kwa abiria, ifikapo kesho majira ya saa 12.30 asubuhi, kampuni hiyo imeeleza sababu za kero hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Udart kupitia msemaji wake, Deus Bugaywa imedai sababu za kukosekana kwa usafiri kwa abiria wa Udart hasa leo tarehe 10 Oktoba 2018 majira ya asubuhi, ni mgomo wa baadhi ya madereva kwa madai ya kupinga kucheleweshewa mishahara yao.
Bugaywa ameeleza kuwa, madereva hao wameharibu mtiririko wa magari baada ya mmoja wao kwa makusudi kuziba njia ya kutokea magari hayo, kitendo kinachohujumu Udart.
“Kawaida mabasi huanza kutoka saa 9 usiku, leo yamechelewa kuanza kazi kwa sababu kuna gari lilienda kupaki kwenye geti la nyuma ambalo mabasi yanatokea na mhusika kutokomea kusikojulikana,” amesema Bugaywa.
Kufuatia hatua hiyo, Udart inafanya uchunguzi wa hujuma hizo kwa kushirikiana na vyombo vya dola kwa ajili ya kubaini wote waliohusika, na uchunguzi utakapokamilika watachukuliwa hatua.
Leave a comment