RAIS wa Tanzania, John Magufuli, amemwapisha James Kaji kuwa Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Kaji aliyekuwa akikaimu nafasi hiyo tangu Agosti 2019 baada ya Rogers Sianga kustaafu, ameapishwa leo Jumatatu tarehe 6 Julai 2020 Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.
Kiapo cha Kaji kimefanyika muda mfupi baada ya Rais Magufuli kumaliza kuwaapisha wakuu wa mikoa na Katibu Tawala pamoja na kushuhudia wakuu wa wilaya wakiapishwa.
Katika hafla hiyo, Rais Magufuli akizungumza masuala mbalimbali ikiwemo operesheni aliyoifanya Kaji Wilaya ya Arumeru Mkoa wa Arusha na kukamata bangi huku akihoji viongozi wa eneo hilo kutoliona.
Rais Magufuli alisema, alimwona Kaji katika moja ta televisheni akiongoza kikosi katika kijiji cha Meru ambacho walikamata bangi.
Alisema haiwezekani Kaji atoke Dodoma aende Meru kukamata wakati eneo hilo kuna viongozi wanaopaswa kusimamia ulinzi na usalama.
Kutokana na hilo, Rais Magufuli pale pale akamwagiza Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro na Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa, Diwani Athuman waliokuwepo kuwaondoa, Mkuu wa Polisi wa Wilaya hiyo (OCD), Mkuu wa Usalama wa Wilaya na wale wote wenye jukumu la kusimamia usalama kwa kushindwa kutotimiza wajibu wao.
Rais Magufuli alisema, ikiwezekana si kuwahamisha tu bali hata kuwashusha vyeo vyao.
“…na wewe (Kaji) leo naku- confirm (nakuthibitisha) kwa sababu umefanya kazi nzuri, mimi nataka mambo yaonekane, inasikitisha mpaka dawa za kulevya mtu atoke Dar es Salaam akayaone wakati mkuu wa mkoa yupo, mkuu wa wilaya yupo, ODC yupo, watendaji wengine wapo,” alisema Rais Magufuli.
Leave a comment