MBUNGE wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), katika jimbo la Singida Mashariki, Tundu Lissu, anaendelea “kumwaga sumu,” katika nchi kadhaa Ulaya na Marekani.
Anasema, shambulio dhidi yake lilillolenga kuondoa uhai wake, lilipangwa na baadhi ya viongozi wakuu wa serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaandika Mwandishi Wetu … (endelea).
Lissu anasema, “tusidanganyane. Some one very powerful wanted me dead – mtu mmoja mwenye madaraka makubwa alitaka nife.
“…na nimeambiwa na watu ambao sina shaka na maneno yao, kwamba the order was (agizo lilikuwa) akifa…hakuna shughuli bungeni na msimlete Dar es Salaam. Mkimbizeni kijijini kwake mkamzike as soon as possible (haraka iwezekanavyo).
Alitoa kauli hiyo, wakati akizungumza na jumuiya ya Watanzania wanaoishi mjini Washington, Marekani. Lissu yuko Marekani kwa mwaliko wa mashirika kadhaa kueleza kilichomtokea na hali ya kisiasa ilivyo nchini.
Mwanasiasa huyo machachari wa upinzani nchini alishambuliwa kwa risasi na wanaoitwa na serikali, “watu wasiojulikana,” nje ya nyumba yake, Area D, mjini Dodoma.
Alikuwa akirejea nyumbani kutokea bungeni ambako alishiriki mkutano wa asubuhi.
Mwanasiasa huyo ambaye ni Mnadhimu wa Kambi rasmi ya upinzani bungeni na mwanasheria mkuu wa Chadema, alipatiwa matibabu jijini Nairobi na baadaye akahudumiwa na madaktari bingwa wa mifupa katika hospitali ya chuo kikuu cha Luvein, kilichopo nchini Ubelgiji.
Lissu alikwenda Ubelgiji, tarehe 6 Januari mwaka jana.
Akizungumzia kilichotokea na uhusiano wake na baadhi ya viongozi wandamizi serikalini na katika CCM, Lissu anasema, “haina maana kwamba sina marafiki CCM. Hapana. Ninao wengi, tena wengine ni mawaziri na viongozi wandamizi ndani ya chama hicho.”
Anasema, “na kwa mazingira ya kawaida wangekuja Nairobi. Lakini waliitwa kwenye kikao, wakaambiwa hii habari ya Tundu Lissu msiishabikie na tena msithubutu kwenda Nairobi.”
Lissu anasema, “ninahofia kutaja majina. Lakini kuna siku nitayataja; itakapokuwa salama kwao, sio kwangu…mimi ni survivor (mnusurika) wa sixteen bullets (risasi kumi na sita).”
Anasema, “sitaki mtu mwingine yoyote apitie hiyo njia niliyopitia mie. Kuna vitu ambavyo siwezi kuvisema leo kwa sababu sitaki watu wapitie nilipopitia mie! Lakini kuna siku…tutatajana.”
“Nimekaa hospitalini, hakuja kuniona. Watu wa EU (Umoja wa Ulaya) wa East African Desk (dawati la Afrika Mashariki) wakaja hospitalini. Wakaja kuniuliza, balozi wako amekuja hapa, nikawaambia hajaja.
“Wakasema, tunakwenda kumwambia aje, (akikataa) tutamwambia Donald Tusk asimpokee. Donald Tusk ni Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya. Kwa hiyo, Joe Sokoine akaja. Alikuwa ameongozana na maofisa wake,” anasimulia.
Anasema, “ubalozi wenyewe wapo wanne pamoja na dereva ambaye ni Mghana. You can see this dissent guy (unaweza kuona huyu mtu muungwana) anakuja yaani unamuhurumia.
“Mimi mgonjwa nimelazwa mguu umening’inia na uzito wa makilo kadhaa kwa miezi miwili, lakini namuhurumia balozi. Ndani ya mwezi mmoja, amerudishwa nyumbani.”
Lissu anasema, “sasa (Balozi Sokoine), kuna mahali alikwenda kuaga..kwa serikali ya Ubelgiji na kwa ofisa wa serikali ya Ubelgiji. Huyo Ofisa alikuja kuniambia… Joseph Sokoine, broke down inside my office, (alivunjika moyo) na akaanza kulia ofisini.
Leave a comment