Wafuasi wa chama cha African National Congress (ANC) nchini Afrika Kusini, wameandamana jijini Johannesburg, kushinikiza viongozi wao wakatae kuingia katika muungano na chama cha Democratic Alliance, DA. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Hatu hiyo inajiri baada ya chama hicho tawala cha Afrika Kusini kufungua milango ya mazungumzo kwa chama chochote kilichopata viti bungeni kwenye uchaguzi uliopita na kinachonuwia kuunda serikali ya muungano itakayodumu kwa miaka mitano ijayo.
Maandamano haya yametokana na kushindwa kwa chama cha ANC kupata wawakilishi wengi bungeni ambapo sasa kinalazimika kuunda serikali ya muungano na chama au vyama vilivyopata wawakilishi katika bunge la kitaifa. Lethabo Mmpo ni miongoni mwa watu walioandamana jijini Johannesburg wakipinga ushirikiano wa ANC na chama cha DA wanachodai ni chama cha kibaguzi.
“Tuko hapa leo kuwasilisha wasiwasi wetu juu ya kukishirikisha chama cha DA katika serikali ya mseto, hatuamini kuwa kuna nafasi kwa chama cha kisiasa kinachopinga mabadiliko, chama ambacho kinadhani ni kawaida kuchoma bendera ya Afrika Kusini,” amesema.
Wengine wameandamana pembezoni mwa mkutano maalum wa kamati kuu ya kitaifa ya chama tawala ANC, unaoendelea mjini Ekurhuleni.
Esethu Hassane ambaye ni mjumbe wa kamati ya vijana wa ANC taifa alimeungana na waandamanaji waliopiga kambi nje ya mkutano huo.
“Tupo hapa kusema kwamba tunawaunga mkono katika maamuzi yoyote watakayoyachukua pasipo kukihusisha chama cha DA, kinachounga mkono mauaji ya kimbari dhidi ya watu wa Gaza, na kinachounga mkono ubaguzi wa rangi ndani ya Afrika Kusini.”
Japo baadhi ya wafuasi wa ANC hawakitaki DA kihusishwe kwenye serikali ijayo, lakini wachambuzi wa siasa na uchumi Afrika Kusini akiwamo Peter Bigenda wanadai kuwa, kukishirikisha DA kutavutia wawekezaji.
ANC kimeshafanya majadiliano na vyama mbalimbali ili kuunda serikali ya mseto, kikiwemo chama cha DA, EFF, IFP na kwa upande wa chama cha uMkhonto Wesizwe kinachoongozwa Jacob Zuma.
Hata hivyo, Zuma amesema wale ambao hawataki wazungumze kuhusu kumuondoa Rais Cyril Ramaphosa kwenye uongozi wa chama cha ANC hawataki majadiliano na MK.
Hata hivyo, mkutano maalum wa kamati kuu ya kitaifa ya chama tawala ANC ambao leo Ijumaa huenda ukategua kitendawili cha vyama gani vitaunda serikali ya mseto, ambao bado haujamalizika.
Vyama vya kisiasa vina wiki mbili kufanya makubaliano ili kuunda serikali ya muungano kabla ya bunge jipya kuketi na kuchagua rais, ambaye bado anaweza kuwa kiongozi wa ANC Cyril Ramaphosa.
Leave a comment