Kanisa Katoliki Jimbo la Bukoba limemsimamisha kutoa huduma za kichungaji Padri Elipidius Rwegoshora kutokana na tuhuma za kuhusika katika mauaji ya mtoto Asimwe Novart mwenye ulemavu wa ngozi -albino. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Uamuzi huo umetangazwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Bukoba, Jovitus Mwijage kupitia gazeti la Kiongozi linalotolewa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), toleo lake la Juni 21 -27, 2024
Askofu Mwijage amekiri kuwa mtuhumiwa ni padri wa jimbo lake na amemsimamisha kutoa huduma zote za kichungaji mpaka hapo suala lake litakaposhughulikiwa na vyombo vya sheria.
Akinukuliwa na gazeti hilo, Askofu Kaijage ameesema wamehuzunishwa na taarifa ya mauaji ya Asimwe hasa ikizingatiwa Kanisa Katoliki ni walinzi wa kwanza wa uhai wa wanadamu.
Amesema wanaiombea familia yake na kuiombea roho yake ipate pumzio la amani mbinguni.
“Hata hivyo, tumesikia taarifa ya watuhumiwa na mmojawapo akiwa ni Padri Rwegoshora. Ni kweli padri huyo ni wa jimbo Katoliki Bukoba na tumechukua uamuazi wa kumsimamisha kutoa huduma zote za kichugaji mpaka hapo suala lake litakaposhughulikiwa na vyombo vya sheria.
“Baada ya vyombo vya sheria kumaliza kazi yake, ndipo taratibu nyingine za kanisa zitafuata,” amesema Askofu Mwijage.
Asimwe menye umri wa miaka miwili na nusu alinyakuliwa mikononi mwa mama yake na watu wasiojulikana Mei 30, 2024 katika Kijiji cha Bulamula, Muleba mkoani Kagera.
Mwili wa mtoto huyo ulipatikana tarehe 17 Juni 2024 akiwa ameuawa kikatili kwa kukatwa baadhi ya viungo vyake, kisha kutupwa kwenye kalavati katika barabara itokayo Luhanga kwenda Makongora wilayani Muleba.
Aidha, tarehe 19 Juni mwaka huu, Jeshi la Polisi lilitoa taarifa kutoka Jeshi la Polisi nchini ya kukamatwa kwa watuhumiwa tisa akiwamo Padri Rwegoshora ambaye alitajwa kuwa ni paroko msaidizi wa Parokia ya Bugandika.
Watuhumiwa wengine ni pamoja na baba wa mtoto huyo, Novart Venant, mganga wa jadi Desdeli Evarist mkazi wa Nyakahama, Faswiru Athuman, Gozibert Alkadi, Rwenyagira Burkadi mkazi wa Nyakahama wote wakazi wa Nyakahama.
Wengine ni Selemani Selestine na Nurdin Hamada, wakazi wa Kamachumu pamoja na Dastan Kaiza, mkazi wa Bushagara.
Jeshi la polisi lilisema Padri Rwegoshora anatuhumiwa kumshawishi baba mzazi wa marehemu kufanya biashara ya viungo vya binadamu na kwamba yeye ndiye aliyemtafuta mganga wa jadi na kulipia gharama zote za uganga.
Leave a comment