Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan anatarajia kumpokea Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Filipe Jacinto Nyusi kesho tarehe 2 Julai 2024 Ikulu jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Maonyesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu Sabasaba. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Sharifa Nyanga imesema Rais Nyusi anatarajiwa kuwasili nchini leo Jumatatu jioni ambapo atafanya ziara ya Kiserikali ya siku tatu.
Imesema Rais Samia na mgeni wake Rais Nyusi watashiriki mazungumzo ya pamoja ambayo yatajikita katika sekta ya biashara, uwekezaji, ulinzi na usalama na kisha kushuhudia uwekaji saini wa makubaliano katika sekta mbalimbali za ushirikiano.
“Ziara hii itaendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria, kidugu na kidiplomasia uliopo baina ya Tanzania na Msumbiji ambao uliasisiwa na viongozi wetu; kiongozi wa kwanza wa chama tawala cha nchi hiyo (FRELIMO), Hayati Eduardo Chivambo Mondlane na Baba wa Taifa Hayati Julius Kambarage Nyerere.
“Rais Nyusi pia anatarajia kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) siku ya tarehe 3 Julai 2024 ambapo ataambatana na mwenyeji wake Rais Samia.
Rais Nyusi ataondoka nchini tarehe 4 Julai 2024,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment