September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Dk. Rweikiza atangaza donge nono watakaopata DIV I na II shule ya Brilliant

 

MBUNGE wa Bukoba Vijijini (CCM), Dk. Jasson Rweikzia, ametangaza kwamba kwenye mtandao wa shule za St Anne Marie Academy unaominilikia pia shule ya Brilliant ya Kimara Mbezi kwa Msuguri jijini Dar es Salaam, hakuna mwanafunzi atakayefukuzwa shule baada ya wazazi wake kufariki na kushindwa kulipa ada ya kuendelea na masomo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea). 

Alitangaza uamuzi huo mwishoni mwa wiki wakati wa mahafali ya  14 ya kidato cha nne ya shule ya Brilliant iliyoko Kimara Mbezi jijini Dar es Salaam.

Mtandao huo unamiliki shule za St Anne Marie Academy, Brilliant, Rweikiza Nursery and Primary na Sunshine ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Dk. Rweikiza alisema shule hizo ziliwahi kupoteza wazazi 93 kwasababu mbalimbali na kusababisha baadhi ya wanafunzi kuacha masomo kwa kukosa ada hali ambayo alisema imeilazimu shule hiyo kuwapa msamaha wa ada wanaofiwa.

“Tumekuwa tukipoteza wazazi wengi na mwezi huu pekee tumepoteza wazazi watatu na hali hii imekuwa ikiathiri sana wanafunzi kitaaluma na wengine kuacha shule kwa kushindwa kulipa ada lakini kuanzia sasa hakuna atakayefukuzwa shule kwa kukosa ada baada ya mzazi wake kufariki,” alisema.

“Kama yuko darasa la kwanza na amefiwa na mzazi wake ataendelea kusoma mpaka darasa la saba na kama ni sekondari ataendelea mpaka kidato cha nne,” alisema Dk. Rweikiza.

Dk. Rweikiza alisema katika mpango wa kuinua taaluma shuleni hapo wameaandaa zawadi mbalimbali zikiwemo fedha taslimu kwa awatakaofanya vizuri kwenye masomo yao na ziara za kimasomo kwenye mbuga mbalimbali za wanyama.

Alisema mwanafunzi atakayepata daraja la kwanza atapata sh 600,000 na atakayepata daraja la II atapata Sh 200,000 na kwamba lengo ni kuhakikisha hakuna daraja la nne wala daraja la tatu shuleni hapo.

Mkuu wa shule ya Brilliant, Edrick Phillemon alisema wahitimu hao wa kidato cha nne wameandaliwa vizuri kitaaluma na wanatarajiwa kufanya vizuri kwenye mitihani yao na kwamba ana uhakika wa kupata daraja la kwanza na la pili.

“Tuna uhakika wa kufanya vizuri kwani ukiangalia historia ya shule ya Brilliant huwa haipati daraja la nne wa daraja 0, mara nyingi tunafaulisha kwa daraja la kwanza na la pili,” alisema.

Alisema wanafunzi hao wamewezeshwa kufikia hapo na walimu wenye taaluma na uzoefu wa kutosha huku akimshukuru Mkurugenzi wa shule hizo, Dk. Rweikiza kwa kuendelea kufanya maboresho ya miundombinu ya shule hiyo

.Alisema Dk. Rweikiza amewawezesha kupata maabara iliyosheheni vifaa vya kutosha, vifaa vya kufundishia kama vitabu, projekta, mashine ya kudurufia, maji safi, ulinzi na huduma bora za afya.

Kwenye maonyesho ya kitaaluma shuleni hapo, wahitimu wa kidato cha nne wa shule hiyo walitia fora kwa namna walivyoweza kuelezea masomo ya baiolojia na uhandisi wa umeme kana kwamba ni wakufunzi waliokwisha kuhitimu  kwenye masomo hayo.

Mbunge wa Kibamba (CCM), Issa Mtemvu ambaye alikuwa mgeni rasmi alimpongeza Dk. Rweikiza kwa namna anavyoisaidia serikali kuwekeza kwenye elimu hivyo kuwafanya watoto wengi wa kitanzania kupata elimu bora.

“Nimetembelea maeneo ya shule hii kwa kweli nimefurahishwa na namna mheshimiwa Rweikiza alivyowekeza kwenye miundombinu yake, shule imesheheni vifaa vya kutosha kwa kufundishia kwa kweli lazima tumpongeze Dk. Rweikiza anafanya mambo makubwa sana kwenye nchi hii,” alisema Mtemvu.

About The Author