July 14, 2025

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

NBC yazindua Msimu wa Pili wa Kampeni ya NBC Shambani kuhamasisha kilimo cha kahawa Ruvuma

 

BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imetambulisha msimu wa pili wa kampeni yake ya ‘Shinda Mechi Zako Kinamna Yako na NBC Shambani’ mkoa wa Ruvuma ikilenga kuchochea kasi ya uzalishaji wa zao la kahawa mkoani humo hususani wilaya za Mbinga na Nyasa kupitia huduma mahususi na zenye upendeleo kwa wakulima wa zao hilo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Ruvuma … (endelea).

Ikitambulishwa kwa mara ya pili mkoani humo, kampeni hiyo inakwenda sambamba na mafunzo ya huduma mbalimbali zinazotolewa na benki ya NBC kwa wadau wa kilimo ikiwemo huduma ya bima ya mazao na bima ya afya, uwakala, huduma za kidigitali, mikopo ya zana za kilimo na pembejeo, ujenzi wa maghala pamoja na kuwasaidia wakulima shughuli mbalimbali zinazohusiana na maandalizi ya msimu wa uzalishaji na masoko ya mazao yao.

Hafla ya utambulisho wa kampeni hiyo ilifanyika mwishoni mwa wiki wilayani Mbinga, ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Kisare Makori huku ikihudhuriwa na viongozi wengine waandamizi wa wilaya hiyo pamoja na wadau mbalimbali wa zao la kahawa wakiwemo viongozi vya ushirika na wakulima.

Wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa Kitengo cha Mikakati wa Benki NBC, Msafiri Shayo aliwaongoza maofisa wengine wa benki hiyo akiwemo Meneja wa Benki ya NBC Kanda ya Pwani Bi Zubeider Haroun na Mkuu wa kitengo cha wateja wadogo wadogo na wakulima kutoka Benki ya NBC, Raymond Urassa.

Akizungumzia kampeni hiyo, DC Makori pamoja na kuipongeza benki hiyo kwa kutoa kipaumbele kwa wakulima nchini kupitia huduma zake, alisema ujio wa kampeni hiyo wilayani mwake ni ukombozi muhimu kwa wakulima wa kahawa wanaohitaji upendeleo maalum wa huduma za kifedha na kwamba serikali imejipanga kuhakikisha dhamira ya benki hiyo inafanikiwa.

“Zaidi nimefurahi kusikia kupitia kampeni hii wakulima wanaweza kupata mikopo ya vitendea kazi muhimu kama vile matrekta na zana nyingine za kisasa za kilimo, pembejeo za kilimo na mikopo ya malipo ya awali kwa wakulima.’’

“Pia huduma za bima za afya na kilimo zinazotolewa na NBC ni muhimu sana kwa wakulima, hasa katika kukabiliana na changamoto za kiafya kwao binafsi na familia zao na kujilinda dhidi ya hasara zitokanazo na majanga ya asili ambayo yamekuwa yakiathiri mazao yao,’’ alisema.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Msafiri alisema kampeni hiyo ni sehemu ya muitikio wa benki ya NBC kufuatia wito wa Serikali wa kuchangia katika kufanikisha agenda 10/30 ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo kutoka asilimia 5 hadi 10 ifikapo mwaka 2030.

“Sambamba na uzinduzi wa kampeni hii kwa wakulima wa zao la kahawa wilayani mbinga, pia tunatoa huduma mbali mbali kwao ikiwemo, ufunguaji wa akaunti za wakulima, ambazo hazina makato ya mwezi, huduma za mikopo kwa mkulima mmoja mmoja kwa ajili ya zana za kilimo kama matrekta na mikopo kwa vyama vya ushrika (AMCOS/Union) kwa ajili ya pembejeo zao,’’ alitaja.

Kupitia kampeni hiyo benki ya NBC inatoa huduma za bima ya afya kwa wakulima na huduma za bima ya kilimo inayotoa fursa kwao kulipwa fidia pindi mazao yao yatakapoathiriwa na majanga mbalimbali yakiwemo yale ya asili.

Akifafanua zaidi kuhusu kampeni hiyo Bw Urassa alisema inawalenga wakulima wote wakiwemo mmoja mmoja, vyama vikuu vya ushirika na vyama vya msingi (AMCOS) ambavyo vitapitisha fedha za mauzo kwenye akaunti za NBC Shambani.

“Kupitia kampeni hii ambayo kwa mwaka huu tunaizindua kwa mara ya pili hapa mkoani Ruvuma mahususi kwa wilaya za Mbinga na Nyasa, wakulima wataweza kujishindia vitendea kazi mbali mbali kama vile ‘spray pumps’ ( pampu ya kupulizia dawa) na piki piki. Upande wa AMCOS na UNION watapata fursa ya kujishindia maguta kwa ajili ya usafirishaji wa mazao yao,’’ alitangaza.

Wakizungumza kwa niaba wakulima hao, Mwenyekiti wa AMCOS ya Kibandai Bi Vestina Nombo pamoja nae Katibu wa Kipowolo AMCOS, Matius Kapinga pamoja na kuishukuru na kuipongeza benki hiyo kwa kampeni hiyo muhimu, walionyesha kuvutiwa na huduma za bima za afya na bima za kilimo kutokana na hitaji kubwa walilonalo wakulima hao kwenye masuala huduma bora za kiafya kwa ajili yao na familia zao huku pia wakiitaja huduma ya bima ya kilimo kama suluhisho sahihi dhidi ya athari zitokanazo na majanga mbalimbali yanayoathiri mazao yao.

 

About The Author

error: Content is protected !!