October 1, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Karume kiongozi misheni ya SADC uangalizi wa uchaguzi Msumbiji

 

RAIS Mstaafu wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, amewasili jijini Maputo, Msumbiji kwa ajili ya kuongoza, Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC SEOM), katika Uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Msumbiji unaotarajia kufanyika tarehe 09 Oktoba, 2024. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea) .

Karume aliwasili jijini Maputo jana baada ya kuteuliwa kuongoza misheni hiyo na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC (Organ), kuanzia mwezi Agosti, 2024 hadi Agosti 2025.

Taarifa iliyotolewa leo na Wizaya ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imesema Alhamisi tarehe 03 Oktoba 2024, Karume atazindua rasmi misheni hiyo.

Imesema kwa kushirikiana na wajumbe wa Troika (Tanzania, Zambia na Malawi), Karume anatarajia kukutana na wadau mbalimbali wa uchaguzi ikiwemo Tume ya Uchaguzi ya Msumbiji (CNE), Mabalozi wa Nchi za SADC waliopo Msumbiji, Vyama vya siasa, Asasi za Kiraia, Taasisi za Kidini na Vyombo vya Habari.

“Tarehe 11 Oktoba 2024, Karume anatarajiwa kutoa taarifa ya awali ya Misheni ya SADC baada ya zoezi la uchaguzi nchini Msumbiji kukamilika,” imefafanua.

About The Author