September 23, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Mbowe, Lissu, Lema wakamatwa kwenye maandamano Dar

 

JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata, Freeman Mbowe Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Makamu wake, Tundu Lissu, Godbless Lema katika maandamano yaliyopangwa kufanyika leo jijini hapa. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).

Mbali na viongozi hao pia Polisi wamemkata ni Rhoda Kunchela, Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Katavi na wafuasi wengine 11 wa chama hicho.

Jumanne Muliro, Kamanda wa Kanda hiyo, akizungumza na waandishi wa habari amesema kuwa wamewakamata viongozi hao baada ya kukaidi katazo la jeshi hilo lililotoa kwa madai kuwa maandamano hayo hayakuwa ya amani.

Muliro amesema kuwa jeshi hilo limefuatilia kwa ukaribu matamko ya viongozi wa Chadema limegundua kuwa hayakuashiria kuwa maandamano hayo yatakuwa ya amani.

Chadema kilipanga kufanya maandamano ya amani kupaza sauti dhidi ya mauaji na utekwaji wa watu unaoendelea nchini.

Chama hicho kilipanga kufanya maandamano hayo kuanzia katika vituo viwili, Magomeni Mataa na Ilala Boma na kuhitimishwa kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja.

Jeshi la Polisi lilitawanya maskari wake kwenye mitaa mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam na kuimarisha ulinzi Magomeni na Ilala Boma.

About The Author