September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Ombi la wakili wa utetezi kesi ya wanandoa kujeruhi lagonga mwamba

 

Na

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam imekataa ombi la wanandoa Bharat Nathwan (57) na Sangita Bharat (54) la kutaka shahidi Kiran Ratilal awasilishe kipande kifupi cha video (clip) kinachoonesha alivyotumbukizwa kwenye ndoo ya mchanganyiko wa saruji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Nathwan na Sangita Bharat (54) wanaoishi Mtaa wa Mrima – Kisutu, jengo la Lohana Dar es Salaam wanatuhumiwa kwa mashtaka manne likiwemo la kujeruhi waliyoyatenda Julai 21,2023 kinyume cha sheria.

Ombi hilo liliwasilishwa jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Aaron Lyamuya na Wakili wa Utetezi Edward Chuwa kwa niaba ya wateja wake, wakati Kiran Lalit Ratilal alipokuwa akiulizwa maswali ya dodoso kutokana na ushahidi wake aliyoutoa dhidi ya washtakiwa hao.

Wakili Chuwa alimuuliza Kiran Lalit Ratilal ambae ni shahidi wa nne katika kesi hiyo, kama ni kweli kwenye ushahidi wake alidai kuwa anayo clip inayoonesha alivyotumbukizwa kwenye ndoo hiyo na upo tayari kuitoa, alidai ni kweli anayo, lakini kwa wakati huo hana.

“Kwa hiyo umeomba kuitoa mahakamani kama kielelezo kutokana na maelezo yako uliyoyatoa,”alidai Wakili Chuwa

Baada ya Chuwa kudai hivyo, Hakimu Lyamuya alimueleza kuwa shahidi hakuomba kutoa kipande hicho, lakini Wakili Chuwa aliendelea kudai kuwa wanataka itolewe kama ushahidi.

Hata hivyo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Faraji Nguka alidai kuwa wao hawako tayari kutoa kielelezo hicho, lakini kama Chuwa anataka kufanya hivyo wanaweza kukitoa wao katika utetezi wao kwa kufuata utaratibu.

Wakili Chuwa alidai kuwa kama kuna hatua za kufuata yeye hazikumbuki, ndipo Hakimu Lyamuya aliwaeleza kuwa kuna taratibu za kisheria shahidi kutoa kielelezo wakati wa kipindi cha maswali ya dodoso zinatakiwa zifuatwe.

“Mahakama ya Rufaa katika uamuzi wake katika shauri la Lilian na Jesus ya mwaka 2018 ilitoa utaratibu, kwa hiyo Chuwa kama ulitaka kufanya hivyo ulitakiwa kufuata taratibu kwenye hiyo rufaa imeonesha hatua kwa hatua,”

“Ombi hili linakuja randomly, ombi hili limekataliwa,”alisema Hakimu Lyamuya

Baada ya Hakimu Lyamuya kusema hivyo, Wakili Chuwa alidai kuwa wamemaliza maswali ya dodoso kwa shahidi.

Wakili Nguka alimuuliza shahidi baadhi ya maswali ( Re-examination) kwa ajili ya kutoa ufafanuzi kwa mahakama, alidai upande wa utetezi ulimuuliza sana uhusiano wa mume wake na Hospitali ya Regency, akadai kuwa mume wake sio daktari ni Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo.

Wakili huyo, aliiomba mahakama iwapangie tarehe ya karibu ili walete mashahidi wengine katika kesi hiyo na kudai kuwa wapo tayari kuendelea hata leo.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 30, 2024 saa tatu asubuhi kwa ajili ya kuendelea na usikilizwaji kwa mashahidi wa upande wa mashtaka.

About The Author