September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Wachambuzi: Siasa za machafuko hazikubaliki TZ

 

SIKU chache baada ya viongozi wakuu wa Chadema kukamatwa na Jeshi la Polisi kwa madai ya kukaidi agizo la kupiga marufuku kongamano la maadhimisho ya vijana duniani, wachambuzi wa masuala ya siasa wameonya viongozi hao wa chama hicho kikuu cha upinzani nchini kuheshimu sheria za nchi kwani siasa za machafuko hazina masilahi kwa Taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Wito huo umekuja siku chache baada ya viongozi hao wakiongozwa wa Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe kuachiwa huru huko mkoani Mbeya ambapo wafuasi wa chama hicho wakiratibiwa na Baraza la Vijana Chadema walipanga kufanya kongamano hilo juzi Jumatatu.

Hayo yanajiri baada ya Kamishna wa Oparesheni na Mafunzo, CP – Awadh Haji kubainisha sababu za kipiga marufuku kongamano hilo kuwa ni kauli za viongozi hao wa Bavicha ambazo ziliashiria uvunjifu wa amani.

Akinukuu baadhi ya kauli hizo alipozungumza na vyombo vya habari hivi karibuni, alisema” kuamua hatma ya Taifa la Tanzania na kwamba wapo serious sana kwani kama vijana wa Kenya walijitambua na kuacha uteja kwa serikali.”

Wakizungumzia sintofahamu hiyo iliyojitokeza kati ya viongozi hao wa Chadema na jeshi la polisi, baadhi ya wachambuzi hao akiwamo Proches Chuwa alisema “Tofauti na Kenya, jamii ya Watanzania imeshajipambanua kama wapenda amani na maridhiano, jambo ambalo limeifanya Tanzania kuwa mfano wa kuigwa wa amani na utulivu barani Afrika na duniani kote – miaka na miaka.

“Changamoto kubwa katika historia ya Tanzania, ikiwemo kupigania uhuru, zilitatuliwa bila kumwaga damu. Amani na Utulivu umeiwezesha nchi ipige hatua kubwa za kimaendeleo ambazo yasingewezekana kama Taifa lingekuwa kwenye machafuko. Kutamani machafuko na umwagaji damu unaondelea nchini Kenya utokee Tanzania, ni jambo linalopaswa kukemewa kwa nguvu zote,” alisema.

Kwa upande wake, mchambuzi maarufu wa masuala ya siasa, Mashaka N’kindikwa (Kijana mzalendo) alisema tangu aingie madarakani, Rais Samia amekuwa akihubiri maridhiano na umoja wa kitaifa na ameitekeleza kwa vitendo falsafa yake ya 4R kwa kuruhusu mikutano ya siasa, kushiriki mkutano wa Chadema.

Amesema hakuna Rais mwingine wa Tanzania amewahi kufanya sanjari na kuweka mazingira ya usalama na ustahimilivu wa kisiasa ambao yamepelekea wanasiasa wa upinzani kama Tundu Lissu na Godbless Lema kurudi nchini kuendelea na shughuli zao za kisiasa kwa uhuru mkubwa.

Hata hivyo, amesema Jeshi la polisi lilipaswa kuwakamata watuhumiwa walioandika au kutoa kauli hizo za kichochezi badala ya kukamata wafuasi wote zaidi ya 520.

About The Author