September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Wakulima watakiwa kuchangamkia fursa za kibenki kuchangia pato la Taifa

 

WAKULIMA nchini wameshauriwa kuchangamkia fursa mbalimbali zinazotolewa na taasisi za kilimo pamoja na kibenki zinazolenga kuwawezesha kukuza mnyororo wa thamani katika sekta na hatimae kuchangia pato la taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).

Hayo yameelezwa mkoani Dodoma katika maonesho ya kilimo na ufugaji maarufu nane nane na wadau wa fedha na kilimo wakati Naibu waziri wa Kilimo, David Silinde akishuhudia utiaji saini mkataba wa mashirikiano (MOU) kati ya taasisi tatu.

Taasisi hizo ni EQUITY Benki, taasisi ya biashara ya PASS na taasisi ya MCODE zenye lengo la kuboresha maisha ya watanzania hasa wakulima.

Akizungumza mara baada ya utiaji saini makubaliano hayo na Meneja mkuu wa biashara wa benki ya Equity, Leah Ayoub amesema mkataba huo unalengo la kuboresha maisha ya watanzania hasa wakulima walioko vijijini wanaohitaji kupata huduma za kifedha hususani mikopo lakini hawana dhamana za kupata mikopo. Amesema makubaliano hayo yatawawezesha kupata dhamana za mikopo pasipo gharama yeyote

Naye Mkurugenzi wa biashara kutoka taasisi ya PASS, Adam Kamanda ameeleza kuwa mikataba hiyo ni kwa ajili ya uendelevu kibiashara ambapo watawasaidia wakulima kulima kisasa ili kuongeza tija katika mazao yao na kukuza mnyororo wa thamani kwenye sekta ya kilimo.

Amesema mpaka sasa wamefikiwa wakulima 30,000 na lengo ni kufikia watu zaidi ya 100,000.

Naye Mkurugenzi mtendaji wa Taasisi inayotekeleza mradi wa kuwawezesha wakulima wadogo kupata usaidizi wa kifedha MCODE, Slaiton Kaberege amesema pamoja na hayo pia wanawezesha wakulima kupata pembejeo, na mpaka sasa wamekwishapata mikopo yenye thamani ya Sh 20 bilioni wakiwa na vikundi 1,000 kwenye mikoa sita.

Benki ya Equity inaamini kupitia uwezeshaji wa wakulima wadogo wadogo walio katika vikundi kutaiwezesha benki kufikisha huduma za kifedha kwa wananchi wengi zaidi hivyo kutimiza adhima ya serikali ya kuboresha sekta ya kilimo ambayo imeajiri watu wengi na yenye mchango mkubwa zaidi katika pato la taifa.

Ni dhamira ya Benki ya Equity kufanya kazi na wadau wote wenye malengo na maono yanayoendana na Serikali katika kuhakikisha inachangia juhudi za serikali kwenye sekta ya kilimo hasa hasa Agenda 2030.

About The Author