September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Mfanyabiashara akata rufaa mfanyakazi wa CRDB kuachiwa huru

MFANYABIASHARA Deogratus Minja amewasilisha kusudio la kukata rufaa kupinga hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam ya kumuachia huru mfanyakazi wa Benki ya CRDB, Ibrahim Masahi (40) ambae anatuhumiwa kumjeruhi na nyundo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Inadaiwa kuwa Masahi alimpiga na nyundo jirani yake Minja na kumsababishia kupata madhara makubwa ya mwili mwake kwa madai kuwa kwanini alikwenda kumshtaki serikali za mtaa kwamba anatililisha maji machafu.

Minja amefikia hatua hiyo ya kukata rufaa, baada ya kuona mapungufu katika hukumu hiyo kwa madai kuwa ushahidi aliyoutoa mahakamani hauendani na hukumu iliyosomwa.

Hukumu iliyotolewa na Hakimu Mkazi, Amos Rweikiza amesema kuwa ushahidi uliyotolewa na mashahidi wanne wa upande wa mashtaka haukuweza kuthibitisha kesi bila kuacha shaka lolote na sheria iko wazi kwamba Jamhuri ndiyo wanaotakiwa kuthibitisha kesi.

“Ushahidi uliyotolewa na Minja ni kweli alijeruhiwa na aliweza kuonesha majeraha yake mbele ya Mahakama na pia hata daktari aliyemchunguza alieleza jinsi mlalamikaji alivyokuwa amejeruhiwa kwa kuvunjika bega,”amesema Hakimu Rweikiza

Amesema mahakama ilijiuliza kama mlalamikaji aliweza kumtambua mshtakiwa?, kwa sababu ushahidi unaonesha tukio hilo lilitokea usiku na mlalamikaji alidai alipigwa akadondoka chini ndipo akamgeukia akamtambua mlalamikiwa.

Amesema kuna haja kutengeneza utambuzi kama alimtambua kwa ufasaha, kwenye ushahidi wa Minja amedai mshambuliaji alisimama
nyuma yake akampiga, kisheria lazima aseme kulikuwa na mwanga kiasi gani ambao ulimsaidia kumtambua.

“Kwenye kutambua mtu aliyeshambuliwa ili aweze kumtambua mtu sawa, lazima aseme ukubwa wa mwanga, kwenye ushahidi wake Minja hakutaja kabisa chanzo cha mwanga ambao alikitumia kumtambua mtuhumiwa,”alisema Hakimu Rweikiza

Hakimu Rweikiza amesema wakati mlalamikaji anaulizwa maswali ya dodoso na Wakili wa Utetezi Nestory Wandiba, alidai kuwa ni tukio hilo lilitokea muda mfupi sana, kwa hiyo suala la utambuzi lazima lielezewe kwa ufasaha.

“Katika ushahidi haikuwekwa wazi kama ni nani alimsaidia mtendewa baada ta tukio kutokea kama ni mama Emma au Fadhili.
Utambuzi uliyofanywa na mtendewa haujakidhi vigezo vya kisheria na umeacha mashaka,”

“Kesi haikuthibitishwa kwa viwango vinavyotakiwa katika ushahidi, utambuzi wa mtendewa hakuwa sawasawa kulitakiwa kuwepo na shahidi mwingine ambae angelionesha hilo,”alisema

Masahi alikuwa akituhumiwa kwamba Januari 11, 2023 akiwa eneo la Mbezi Msakuzi ndani ya Wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam alimshambulia na kumjeruhi Deogratus Minja.

About The Author