February 4, 2026

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

NBC yang’ara Tuzo za Mwajiri Bora Programu ya Mafunzo kwa Vitendo

BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) leo imepokea tuzo ya Mwajiri Bora katika Programu ya Mafunzo kwa Vitendo (Internship Program)  kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano kupitia Kitengo cha Huduma za Ajira ikiwa ni utambuzi wa jitihada za benki hiyo katika kuwapatia fursa za ‘Internship’ na kuwaajiri wahitimu kutoka vyuo vikuu mbalimbali kupitia programu ya mafunzo ya Uzoefu wa kazi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Tuzo hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam kwenye Mkutano wa waajiri wanaotekeleza programu ya mafunzo ya Uzoefu wa kazi. Tuzo hiyo imekabidhiwa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Rahma Kisuo (Mb).

Hafla hiyo ilihusisha pia uwepo wa viongozi wengine waandamizi wa serikali akiwemo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bi Zuhura Yunus, viongozi, maofsa wa OWM-KAM,  wawakilishi wa taasisi mbalimbali.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Rasilimali Watu Benki ya NBC, Grace Mgondah aliwaongoza maofisa wa benki ya NBC kwenye tukio hilo.

Akizungumzia hatua hiyo, Mgondah alisema  tuzo hiyo inatokana na  jitihada za benki hiyo katika kufanikisha program hiyo ya mafunzo ya Uzoefu wa kazi  (internship) ambapo katika kipindi cha miaka mitano ya utekelezaji wa mpango huo benki hiyo imetoa  ajira  za kudumu takribani 136 miongoni mwa wahitimu kutoka vyuo vikuu mbalimbali waliopata fursa ya kufanya mafunzo ya Uzoefu wa Kazi kwenye benki hiyo.


“Kila mwaka wahimitimu takribani 800,000 hadi 1,200,000 wanahitimu na kutafuta ajira hapa nchini. Hata hivyo changamoto kwao ni pamoja na wengi wao kukosa ujuzi na uzoefu wa kutosha kwenye taaluma. Mafunzo haya yamekuwa ni msaada mkubwa sana kwa wahitimu hawa kwa kuwa yamekuwa yakiwajenga zaidi hususani katika kuwajengea ujuzi, Uzoefu na maadili ya kazi pamoja na kuwapa mtazamo chanya juu ya ulimwengu wa kazi,” alisema.

Kwa mujibu wa Mgondah, pamoja na ajira zilizotolewa kwa wahitimu hao, benki hiyo imeweza kuwasaidia  wahitimu wengine wengi kupata ajira kwenye taasisi mbalimbali ambapo wamekuwa wakifanya vizuri zaidi  huku akiahidi kwa niaba ya benki hiyo kuendeleza ushirikiano huo na serikali katika kutekeleza mpango huo kwa faida ya wahitimu wengi zaidi.


“Hivyo,  nawashauri wahitimu wote kujiandikisha kwenye mfumo wa OWM-KAM ili weweze kuunganishwa na fursa mbalimbali zilizopo kwa waajiri. Link yao ni jobs.kazi.go.tz.” aliongeza

About The Author

error: Content is protected !!